Social Icons

rss feed facebook twitter google plus linkedin youtube email

Thursday, January 9, 2014

Mapigano makali yaendelea nchini Sudan Kusini


Mapigano makali yaendelea nchini Sudan KusiniMapigano makali yanaripotiwa kuendelea kati ya wanajeshi wa serikali ya Sudan Kusini na waasi wanaoongozwa na makamu wa zamani wa rais Riek Machar.
Msemaji wa jeshi la Sudan Kusini Philip Aguer amesema siku ya Jumatano walipambana vikali na waasi katika kupigania udhibiti wa Bor, mji mkuu wa Jimbo la Jonglei. Aidha mapigano yanaripotiwa kuendelea katika jimbo lenye utajiri wa mafuta la Nile ya Juu. Msemaji wa waasi Youhani Musa Pauk amesema hakutakuwa na usitishaji mapigano hadi pale serikali ya Juba itakapowaachilia huru wanasiasa wapinzani ambao walitiwa mbaroni punde baada ya machafuko kuibuka wiki tatu zilizopita. Huku hayo yakijiri wapatanishi kutoka jumuiya ya kieneo ya IGAD wanasema mazungumzo baina ya pande hasimu yanaendelea vizuri na kwamba Rais Salva Kiir wa Sudan Kusini amesitiza kuwa mgogoro wa sasa ni wa kisiasa na kwamba anaunga mkono suluhisho la kisiasa. Machafuko nchini Sudan Kusini yalianza Disemba 15 katika mji mkuu Juba, pale wanajeshi wanaoaminika kuwa watiifu kwa Riek Machar, walipojaribu kuipindua serikali ya Rais Salva Kiir. Uhasama wa kisiasa nchini humo ulianza mwezi Julai mwaka jana baada ya Kiir kumfuta kazi Machar. Kiir ni kutoka kabila la Dinka ambalo ndilo lenye nguvu zaidi na Machar ni wa kabila la Nuer.

No comments:

Post a Comment