Social Icons

rss feed facebook twitter google plus linkedin youtube email

Friday, June 8, 2012

muungano huu unahitaji dawa mseto

Mandhari nzuri ya mji wa Zanzibar yenye kupendeza na kuwavutia watalii wengi kutoka nchi mbali mbali huharibika kwa muda mchache kutokana na vurugu zinazotokea iwapo vurugu hizo zitashindwa kuthibitiwa


Upepo mbaya ulivuma sio ule wa kimbunga, hapana huu ulikuwa ni upepo uliotaka kuyumbisha chombo chetu ili kienda mrama,lakini tumevuka salama katika mtihani tulioupata wa vurugu zilizotokea. Madai ya Wazanzibari ni madai ya miaka mingi tangu kuasisiwa kwa Muungano wa Tanganyika na Zanzibar. Muungano huu umeelzwa katika tafiti nyingi za wasomi na wasiokuwa wasomi kwamba muundo wake ndio wenye matatizo.
Kuwepo kwa fursa ya kutoa maoni katika Tume ya katiba ni jambo muhimu hasa kwa Wazanzibari ambao walikuwa na dukuduku la siku nyingi wakilalamika bila kusikilizwa maana wasilikizaji ndio wale wale wanaolalamiwa.
Wananchi walio wengi wamejizatiti kwenda kwa wingi wakati Tume itakapoanza kukusanya maoni, lakini kuna jambo ambalo linazungumzwa sana katika maeneo ya Unguja na Pemba kuhusu Zanzibar kupiga kura ya maoni kwanza kabla ya kuingia katika utoaji wa maoni ya katiba mpya.
Nilibahatika kuwasilikiza viongozi wa Uamsho katika mkutano wao waliofanya msikiti wa Mbuyuni Ijumaa iliyopita, walieza mambo kadhaa wa kadha,kubwa walilonishtua ni kuwa ikiwa maoni ya wananchi wa pande mbili hizi za Muungano yakitofautiana uamuzi utakuwaje?
Hili ni swali la msingi kabisa, Uamsho walisema ikiwa Wazanzibari kwa mfano wanataka Serikali moja, watu wa Tanzania Bara wao wanataka mbili au ikawa kinyume chake, maamuzi yatakuwavipi au Tume inapendekeza inavyoona inafaa?
Kwa kuondoa shaka hiyo, Sisi ndio maana tunashikilia kuwepo kwa kura ya maoni hapa Zanzibar kwanza kuwauliza Wazanzibari kuhusu Muungano” ndivyo alivyokuwa akieleza Kiongozi wa Jumuiya ya Maimamu Zanzibar Sheikh Farid Hadi Ahmed.
Je viongozi Zanzibar wanaogopa kitu gani kura ya maoni mbona imeshawahi kufanyika na sio jambo geni machoni mwao, wanahofu ya nini maana atafutwi mshindi katika hili.
Wanaotaka kura ya maoni wanataka kukijenga chombo chao kiwe madhubuti kwa uhakika wa safari wanayotaka kwenda katika maoni ya katiba mpya maana chombo kikitolewa chelezoni na kutiwa majini kitaweza kuhimili misukosuko ya bahari.
Au ndio kuna shinikizo la watu wanaotetea mfumo dhaifu wa Serikali mbili, wengine tuliwasikia zilipotokezea vurugu walitumia fursa hiyo kueleza mambo ya ovyo, wapo walijikweza kisiasa, wapo waliotafuta umaarufu,lakini pia wapo walioendeleza misimamo yao.
Sote tumesikia alivyoambiwa Waziri wa Katiba na Sheria,Abubakar Khamis Bakar ajiuzulu kwa kisa cha watu wanaodhaniwa kuwa Uamsho kufanya vurugu, hivi kuna uhusiano gani na Waziri huyo?
Waliofanya vurugu hawakutumwa na Serikali, wala kiongozi mwengine yoyote yule hivyi,sioni mantiki ya kumtaka Waziri huyu kujiuzulu au labda wanaomtaka ajiuzulu wanatatizo binafsi sawa,lakini katika vurugu zilizotokea hakuna wala sioni sababu ya yeye kuwajibika.
Pengine Rais wa Zanzíbar Dk. Ali Mohammed Shein akatofautiana na wanaotaka Waziri Abubakar ajiuzulu,akisema akaulizwe aliyesema hayo,lakini yeye hana la kueleza kwa maana nyengine Dk Shein haoni sababu ya kutakiwa Waziri wake kuachia ngazi.
Mnyonge mnyongeni haki yake mpeni, katika hili Waziri Abubakar kaonewa sana kwani hausiki na jambo lolote mbona wale vijana wenu waliposema wanazopesa za kununua nondo za kuwashambulia Uamsho hakuna kiongozi aliyetakiwa kujiuzulu kwa matamshi ya vijana wao kuchochea na kutaka kuvunja amani?
Ni lazima kuelewa kuwa matatizo ya kijamii hayawezi kutatuliwa na hisia za mtu mmoja tena aliyepitwa na wakati anayetumia Nokia ya tochi asiyeweza kuunganishwa na mitandao ya kijamii ya facebook, twitter ambaye anategemea mawasiliano ya mbiu ya mgambo au baragumu katika zama hizi za utandawazi.
Mara nyingi panapotokeza tatizo katika jamii basi sheria ambazo lengo kuu ni kupambana na wahusika, badala yake matatizo ya kijamii yatatatuliwa na sayansi au mfumo ulio sahihi utakao hakikisha haki ndiyo inayotawala katika jamii.
Kelele za kero za Muungano zimeshawachosha Wazanzibari kuzisikia maana kukosekana kwa mfumo sahihi wa muundo wa Muungano ndiko kunakosababisha leo tuanze kujadili upya suala la aina gani ya mfumo wa Muungano ulio muafaka na kwa ajili hiyo, Wazanzibari wengi wanataka Muungano wa mkataba.
Tunaelewa katika kipindi chote cha utawala wa CCM suala la Muungano limeonekana kama ni mwiko kulijadili, halizungumziki, woga umetawala, kumbe wamesahau kuwa wakati unabadilika, kizazi cha leo sio kile cha akina hewala bwana.
Ndio maana yamezuka makundi ya kijamii yanayopigania haki ya kujieleza na ile ya kuamua mambo watakavyo maana katiba ya Zanzibar inasema mamlaka ya uendeshaji wan chi yatakuwa kwa wananchi wenyewe vipi leo waonekane kituko wanapotaka mfumo wa muundo wa Muungano ubadilike?
Vijana hawana kazi, hawana bazi, wapo wapo tu hawana uhakika na wapi watapata chakula cha kutwa hivyo kunapojitokeza fursa kama hizi za madai ya haki hakuna atakayebaki nyuma na ndio maana jaribio la kuwaziba mdomo kuujadili Muungano ni gumu sana pengie ni rahisi Ngamia kupita kwenye tundu la sindano,kuliko Wazanzibari kukatazwa kujadili Muungano.
Leo Wazanzibari wengi wanaponea kuvaa mitumba kuanzia nguo za nje hadi nguo za ndani, chupi, sidiria, soksi na hafu, viatu, vyombo vya nyumbani hivi watu hao wakielezwa kuwa tukiwa na mfumo bora usiokuwa wa kubanana tutapumuwa kwa raha wasikubali?
Makero yamezidi kuota mapembe, hayatibiki kama zilizvyoshindwa zile dawa za kutibu malaria hadi yalipofanyika mabadiliko ya kukubali dawa mseto ya kutibu ugonjwa huo.
Muungano wetu unahitaji dawa mseto itakayokuwa tiba sahihi kwa kuwa na Muungano wa mkataba utakaowaacha Wazanzibari wapumuwe maana miaka 48 wamekuwa katika kitimkim cha kero zisizopatiwa ufumbuzi katika Muungano huu.
Ndio maana kila siku mfumo wa muundo wa Serikali mbili unavyopoteza umaarufu miongoni mwa Wazanzibari kwani watu wengine wanaweza kuanguao kilio, lakini kinachowasukuma kufanya yote hayo siyo ile hali ya roho zao kupenda mabadiliko, bali ni kule kuelemewa na matatizo ya kiuchumi ambayo kimsingi yamesababishwa na mfumo mbaya wa muundo wa Muungano uliodumu kwa miaka 48 sasa.
Kama Muungano ungekuwa wenye mfumo bora,hawa wanaolalamika wekiwemo Uamsho,wanasiasa na wanaharakati wasingekuwa na sababu ya kufanya hivyo, mbona hawalalamiki katika mambo mengine ambayo yamewekewa misingi imara?
Tanzania ilipinga kuharakishwa kwa Shirikisho la kisiasa la Afrika Mashariki kwa madai bado kuna mambo katika Jumuiya yenyewe ya EAC yanayohitajika kuwekwa sawa kama suala la ardhi, ajira na mambo mengine.
Maelezo ya Tanzania ni kwamba ardhi lisiwe katika orodha ya mambo ya Shirikisho la Afrika Mashariki kwa maana nyengine wasiwasi wa Watanzania ni mfumo wa Shirikisho hilo, sasa kwanini Wazanzibari wanapokuwa na wasiwasi na muundo wa Muungano wachukuliwe kuwa ni wakorofi?
Lakini pia kuna mambo mengi katika Jumuiya ya Afrika Mashariki yenye utata, kuna mambo ambayo si ya Muungano,lakini yamejumuishwa katika EAC je uwakilishi wa Zanzíbar utakuwaje?
Mambo ya kilimo,afya, vijana, utamaduni nikiyataja kwa uchache haya kila upande una mamlaka yake ya uendeshaji kwa msingi huo kutakuwa na mgongano wa maslahi maana idadi ya wajumbe inakuwa sawa,Tanzania haiwezi kupeleka kwa mfano Mawaziri wawili wa Kilimo au wa Afya.
Kama kutakuwa na muundo wa Muungano kama ule wa Umoja wa Ulaya ambao unaruhusu kila nchi kuwa na mamlaka yake, Muungano huu utakuwa wenye nguvu katika ukanda wa maziwa makuu.

No comments:

Post a Comment