Social Icons

rss feed facebook twitter google plus linkedin youtube email

Tuesday, June 26, 2012

Hukmu Ya Muziki Katika Qur-aan Na Sunnah

Muziki ni haraam kutokana na dalili dhahiri tulizopewa katika Qur-aan na Hadiyth za Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam).
Baadhi wa watu katika Jamii yetu bado hawajatambua uharamu wa jambo hili, tunasikia wengi bado wanaimba taarabu au miziki mbalimbali, na mara kwa mara unapomnasihi nduguyo Muislamu kuacha maasi haya, jibu mara nyingi huwa: "Tena nyinyi mmezidi! Wapi inasema kuwa nyimbo haramu" Au wengine waliobobea katika maradhi haya hunena: "Mimi yote naweza kuacha lakini nyimbo utaniua", husema hivyo bila ya kujali amri ya makatazo ya Mola Mtukufu ambaye ni Muweza wa kuyaua masikio yake awe kiziwi na asiweze kusikia tena hizo nyimbo.
Inafika hadi Muislam hawezi kulala hadi alazwe kwa muziki, hawezi kula ila muziki uwe unapigwa, hawezi kufanya kazi za nyumbani bila muziki kufunguliwa, hawezi mtu kutembea bila kuwa na walkman au mp3 yake ikicheza, hawezi kufanya kazi akiwa kazini…hawezi kusafiri…hawezi hata kufanya mazoezi ya ndani bila kuwepo na muziki wa kumchochea na kumtia hamasa (kama wanavyoitakidi) ya lile analolifanya kwa wakati huo! ‘Alaa kulli haal, muziki umekuwa ni sehemu kiungo kikubwa cha maisha ya mwanaadam kwa wakati huu!
Hivyo tumeona kuna umuhimu mkubwa wa kuwakumbusha ndugu zetu waepukane na haramu hii ili wajiokoe na ghadabu za Mola Mtukufu, ghadhabu kali ambazo zinafika kumgeuza mtu awe nyani au nguruwe kama tutakavyosoma katika hizi dalili za wazi wazi zenye uhakika.
Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala):

((وَمِنَ النَّاسِ مَن يَشْتَرِي لَهْوَ الْحَدِيثِ لِيُضِلَّ عَن سَبِيلِ اللَّهِ بِغَيْرِ عِلْمٍ وَيَتَّخِذَهَا هُزُوًا أُولَئِكَ لَهُمْ عَذَابٌ مُّهِينٌ))

((Na miongoni mwa watu wapo wanaonunua maneno ya upuuzi, ili wawapoteze watu na njia ya Mwenyezi Mungu pasipo kujua, na wanaichukulia ni maskhara. Hao watapata adhabu ya kuwafedhehesha)) [Luqmaan: 6]

Ibn Mas'uud (Radhiya Allaahu 'anhu) amesema kuhusu Aayah hii "Naapa kwa Allaah hii inamaanisha ni kuimba" [At-Twabariy 20:127]

وعن ابن عباس قال عن آية: ((ومن الناس من يشتري لهو الحديث))، قال :الغناء وأشباهه إسناده صحيح - المحدث: الألباني

Na Ibn 'Abbaas (Radhiya Allaahu 'anhuma) pia amesema kuhusu Aayah: ((Na miongoni mwa watu wapo wanaonunua maneno ya upuuzi)) "Ni nyimbo na maneno ya yanayofanana (ya upuuzi)" [Isnaad Sahiyh kutoka kwa Shaykh Al-Albaaniy]
 
Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Anamwambia Ibilisi:


((وَاسْتَفْزِزْ مَنِ اسْتَطَعْتَ مِنْهُمْ بِصَوْتِكَ وَأَجْلِبْ عَلَيْهِم بِخَيْلِكَ وَرَجِلِكَ وَشَارِكْهُمْ فِي الأَمْوَالِ وَالأَوْلادِ وَعِدْهُمْ وَمَا يَعِدُهُمُ الشَّيْطَانُ إِلاَّ غُرُورًا))

 
((Na wachochee uwawezao katika wao kwa sauti yako, na wakusanyie jeshi lako la wapandao farasi na waendao kwa miguu. Na shirikiana nao katika mali na wana, na waahidi. Na shaytwaan hawapi ahadi ila ya udanganyifu)) [Al-Israa: 64]
Hii inamaanisha ni nyimbo kama ilivyo rai ya Mujaahid katika Tafsiyr ya Ibn Kathiyr]
Vile vile Hadiyth zifuatazo zimedhihirisha uharamu wa nyimbo, ngoma na kila aina ya muziki:


عبدالله بن عمرو بن العاص عن رسول الله صلى الله عليه وسلم انه قال: ((إن الله حرم الخمر والميسر والكوبه وكل مسكر حرام ((إسناده صحيح

و في رواية أحمد قال سفيان: قلت لعلي بن بذيمة: "ما الكوبة؟" قال: "الطبل"
Kutoka kwa 'Abdullaah bin 'Amru ibnul 'Aasw kwamba Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Hakika Allaah Ameharamisha pombe na kamari na kuubah na kila kilinacholewesha ni haram)) [Isnaad yake ni Sahiyh]
Na katika usimulizi mwingine kutoka kwa Imaam Ahmad, Sufyaan amesema: Nilimuliza 'Aliy ibn Budhaymah: "Nini Kuubah?" Akasema: "Ngoma".

 WENYE KUIMBA/KUSIKILIZA MUZIKI WATAGEUZWA KUWA NYANI
NA NGURUWE!

 
 وقال رسول الله صلى الله عليه وسلم: ((ليكونن من أمتي أقوام يستحلون الحر و الحرير و الخمر و المعازف، و لينزلن أقوام إلى جنب علم، يروح عليهم بسارحة لهم، يأتيهم لحاجة، فيقولون: ارجع إلينا غدا، فيبيتهم الله، ويضع العلم، ويمسخ آخرين قردة وخنازير إلى يوم القيامة ((رواه البخاري
 Na akasema Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam): ((Watakuweko watu katika Ummah wangu watakaojaribu kuhalilisha zinaa, uvaaji wa hariri, pombe na muziki. Baadhi ya watu watakuwa pembeni mwa mlima na mchungaji wao atawajia jioni na kuwaomba haja [fulani]. Watasema: "Rudi kesho". Allaah Atawaangamiza usiku, Atawaangushia milima kisha Atawabadilisha waliobakia wawe nyani na nguruwe na watabakia hivyo hadi siku ya Qiyaamah))[Al-Bukhaariy]


Hadiyth hii inatuthibitishia kuwa madhambi yote hayo yako sawa sawa uharamu wake,
kama vile zinaa na pombe ilivyo haramu, basi na muziki pia haramu sawa sawa. Sasa vipi Muislamu aone kuwa muziki sio maasi makubwa ya kujiepusha nayo?
 
Imaam Abu Haniyfah amesema: "Kuimba (nyimbo, ngoma) ni katika madhambi makubwa ambayo inatakiwa Muislamu kujiepusha nayo haraka"
 
Khofu zaidi imuingie Muislamu kuwa anaweza kupata adhabu ya kugeuzwa nyani au nguruwe kwa maasi haya kama tulivyoonywa katika Hadiyth ifuatayo:


 
وقال رسول الله صلى الله عليه وسلم: ((ليشربن أقوام من أمتي الخمر يسمونها بغير اسمها يعزف على رؤوسهم بالمعازف والمغنيات ، يخسف الله بهم الأرض ويجعل منهم قردة وخنازير)) قال الشيخ الألباني- رحمه الله تعالى- : صحيح

 
Na kasema Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam): ((Watu katika Ummah wangu watakunywa pombe wakiipa jina jengine lisilokuwa hilo, miziki itapigwa kwa ajili yao na watakuweko waimbaji wanawake. Allaah Atawadidimiza ardhini na Atawageuza wawe nyani na nguruwe)) [Ibn Maajah na Shaykh Al-Albaaniy ameipa daraja ya Sahiyh]



 GHADHABU ZA ALLAAH KUWAANGAMIZA WAFANYAO MAASI HAYA!


 
Vile vile ghadhabu za Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) ni kali mno za kuangamizwa pindi maasi haya yatakapodhihirika.


 عن عمر بن حصيل عن رسول الله صلى الله عليه وسلم انه قال: ((يكون فى امتى قذف ومسخ وخسف)): قيل يارسول الله ومتى ذلك قال: ((اذا ظهرت المعازف… )) اخرجه الترمذى وصححه العلامه الالبانى

 
Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) kasema: ((Kutatokea katika Ummah huu maafa ya kuteremshiwa mawe kutoka mbinguni, kugeuzwa maumbile ya binaadamu [kugeuzwa kufanywa nyani na nguruwe] na mididimizo [ya ardhi]. Ikaulizwa: Ewe Mjumbe wa Allaah, lini yatatokea hayo? Akasema: ((Itakapodhihirika muziki … )) [At-Trimidhy na ameipa daraja ya Sahiyh Shaykh Al-Albaaniy]

 
 QUR-AAN NDIO NYIMBO YETU

 Muziki na nyimbo humjaza mtu mapenzi makubwa moyoni, zimshughulishe zaidi hadi asiwe na muda wa kusoma maneno ya Mola wake Mtukufu ambayo hiyo ndio inayopasa kuifanya iwe midomoni na moyoni mwetu daima kwa kusoma kwa sauti nzuri ya kupendeza (Tajwiyd) kama tulivyoamrishwa na Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam).



 SAUTI ZA NYIMBO ZIMELAANIWA DUNIANI
NA AKHERA

 قال رسول الله صلى الله عليه وسلم: ((صوتان ملعونان فى الدنيا والاخره مزمار عند نعمه ورنه عند مصيبه)) البزار و صححه العلامه الالبانى

 Na kasema Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam): ((Sauti mbili maluuni [zilizolaaniwa] duniani na Akhera; mizumari katika furaha na kuombeleza katika misiba)) [Al-Baazaar – na Shaykh Al-Albaaniy kaipa daraja ya Sahiyh]
 

 NI SUNNAH KUZIBA MASIKIO UNAPOSIKIA MUZIKI BILA YA KUTAKA

 
عن نافع أنه قال: سمع ابن عمر مزمارا، قال: فوضع أصبعيه على أذنيه، ونأى عن الطريق، وقال لي: يا نافع هل تسمع شيئا؟ قال: فقلت: لا! قال: فرفع أصبعيه من أذنيه، وقال: كنت مع النبي صلى الله عليه وسلم، فسمع مثل هذا! فصنع مثل هذا - حديث صحيح، صحيح أبي داوود وراجع السلسلة الصحيحة للألباني 
Kutoka kwa Naafi'i ambaye amesema, amesikia sauti ya muziki akaziba masikio yake kwa vidole vyake, kisha akamgeuza mnyama wake aliyempanda [arudi asiendelee kwenda sehemu hiyo iliyokuwa na muziki] akasema: "Ewe Naafi'i, umesikia kitu?" Akasema, nikajibu: "Hapana". Akaondosha vidole vyake masikioni mwake akasema: "[siku moja] Nilikuwa na Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) aliposikia kama hivi [muziki] akafanya kama hivi [nilivyofanya mimi yaani kuziba masikio yake asisikie sauti ya mizumari] [Hadityh Swahiyh ya Abu Daawuud  na   Ikiwa katika Silsilatus-Swahiyha ya Shaykh Al-Albaaniy]

 

 
و قال رسول الله صلى الله عليه وسلم: ((لا تصحب الملائكة رفقة فيها كلب ولا جرس)) مسلم
 
Na kasema Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam): ((Malaika hawafuatani na watu wenye mbwa na walio na kengele)) [Muslim]
 
Tanbihi: Ikiwa kengele tu inawakimbiza Malaika, seuze nyimbo, ngoma, mizumari na aina zote za muziki ambazo zinaamsha vishawishi na kuchochea hisia za binaadamu!

 MWENYE KUMPA MWENZIWE TAARIFA AU KUMPELEKA KWENYE MUZIKI ATABEBA DHAMBI ZAKE
NA DHAMBI ZA MWENZIWE!

 Mara nyingi Waislamu wenye kufanya maasi haya wanasabisha wenzao kutumbukia pia katika maasi haya; kuna wanaoalika watu katika shughuli zenye maasi hayo (parties) zenye mchanganyiko wa wanawake na wanaume, wenye kupiga taarabu katika maharusi, na wengine wanaofika hadi kununua kanda (cassettes), CD au Video na kuwapa wenziwao kama zawadi.
 
Watambue wanaoanza kuwahusisha wenziwao na maasi haya kuwa watabeba madhambi yao na ya wenziwao pia na hizo dhambi ataendelea kupata mwenye kuanzisha kila yanaposambaa kwa maelfu ya watu! Ni mzigo mzito kiasi gani atakaoubeba mwenye kumhusisha mwenziwe na maasi haya?

 Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala):


 
((إِنَّا نَحْنُ نُحْيِي الْمَوْتَى وَنَكْتُبُ مَا قَدَّمُوا وَآثَارَهُمْ
وَكُلَّ شَيْءٍ أحْصَيْنَاهُ فِي إِمَامٍ مُبِينٍ))  
((Hakika Sisi Tunawafufua wafu, na Tunayaandika wanayoyatanguliza, na wanayoyaacha nyuma. Na kila kitu Tumekihifadhi katika daftari asli lenye kubainisha))
[Yaasiyn:12]
 
Pia Mtume (Swalla Allahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) ametuambia:

 
((من سن في الإسلام سنة حسنة كان له أجرها وأجر من عمل بها من بعده لا ينقص ذلك من أجورهم شيئاً ومن سن في الإسلام سنة سيئة كان عليه وزرها ووزر من عمل بها من بعده لا ينقص من أوزارهم شيئاً)) خرجه مسلم في صحيحه

 
((Atakayefanya kitendo chema katika Uislam atapata ujira wake na ujira wa yule atakayekitenda baada yake bila ya kupungukiwa thawabu zao. Na atakayetenda kitendo kibaya katika Uislam atabeba (mzigo wa) dhambi zake na dhambi za yule atakayetenda wala hapungukiwi kitu katika (mzigo wa) dhambi hizo)) [Muslim]

 
TAHADHARI NDUGU MUISLAMU! BINAADAMU ATAFUFULIWA
NA AMALI YAKE YA MWISHO!


 Ikiwa ndugu yetu Muislamu ni mpenda muziki sana, basi tunakuomba utahadhari na kauli ya Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) aliyosema:

 

 
عن جابر بن عبدالله قَالَ : سَمِعْتُ النَّبِيَّ صَلَّى اللَّه عَلَيْهِ وَسَلَّمَ يَقُولُ: (( يُبْعَثُ كُلُّ عَبْدٍ عَلَى مَا مَاتَ عَلَيْه)) رواه مسلم

Kutoka kwa Jaabir bin 'Abdullaah ambaye amesema: "Nimemsikia Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) akisema: ((Kila mja atafufuliwa katika hali aliyofia nayo))[Muslim]
 
Je, ndugu Muislamu unayependa muziki, umetafakari vipi utakuwa mwisho wako?

Je, haikuingii khofu katika moyo wako kuwa huenda mwisho wako ukawa ni kuimba nyimbo badala ya kusema "Laa ilaaha Illa Allaah" neno ambalo ukilitaja mwisho wa maisha yako wakati wa kufa utaingia Peponi?

 
KISA CHA KWELI MTU ALIYEFARIKI AKIWA ANASIKILIZA NYIMBO!

Katika moja ya nchi za Ghuba, Kijana mmoja aliyekuwa mpenzi wa nyimbo alikuwa haachi kusikiliza nyimbo katika gari lake. Kila alivyokuwa akikatazwa na wazazi wake na wenziwe waliokuwa wameongoka hakuwa akitaka kusikia nasaha hii. Siku ya ajali yake alitoka akiwa anaendesha gari yake na huku akisikiliza nyimbo ya Ummu Kulthuum 'Hal Ra-al-Hubbu Sukaara' (Je, hakuona mapenzi yanavyolewesha). Alipata maafa mabaya katika ajali hiyo ya gari na ukawa ndio mwisho wake. Kabla ya roho yake kutoka, walijaribu Maaskari wa usalama wa barabarani na waliokuweko kumlakinia (kumsemea atamke 'Laa ilaaha illa Allaah') lakini wapi! Kila akiambiwa aseme 'Laa ilaaha illa Allaah' alikuwa akitamka ''Hal Ra-al-Hubbu Sukaara" "Hal Ra-al-Hubbu Sukaara" na hayo ndio yakawa ni maneno yake ya mwisho akielekea kuonana na Mola wake Mtukufu, na ndio atakayofufuliwa nayo!



Tunamuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Aturuzuku mwisho mwema na tunatumai kuwa ndugu zetu ambao bado wako katika maasi haya, watakaposoma dalili hizi, zitakuwa ni mazingatio kwako na kumkhofu Mola wao Mtukufu wajiepusha na uharamu huu na wabaki katika Radhi Zake Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala)

No comments:

Post a Comment