Social Icons

rss feed facebook twitter google plus linkedin youtube email

Tuesday, June 26, 2012

Madhara Ya Ghiybah (Kusengenya)

Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala):
((وَلاَ تَقْفُ مَا لَيْسَ لَكَ بِهِ عِلْمٌ إِنَّ السَّمْعَ وَالْبَصَرَ وَالْفُؤَادَ كُلُّ أُولئِكَ كَانَ عَنْهُ مَسْؤُولاً))

((Wala usifuate (ukipita ukisema au kuyafanya) usiyo na ilimu (ujuzi) nayo. Hakika masikio, na macho, na moyo hivyo vyote vitaulizwa)) [Al-Israa: 36]  

Na Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala):
 (( وَلاَ يَغْتَب بَّعْضُكُم بَعْضًا أَيُحِبُّ أَحَدُكُمْ أَن يَأْكُلَ لَحْمَ أَخِيهِ مَيْتًا فَكَرِهْتُمُوهُ وَاتَّقُوا اللَّهَ إِنَّ اللَّهَ تَوَّابٌ رَّحِيمٌ))
((Wala msisengenyane nyinyi kwa nyinyi. Je! Yupo katika nyinyi anayependa kuila nyama ya nduguye aliyekufa? Mnalichukia hilo! Na mcheni Allaah. Hakika Allaah ni Mwenye kupokea toba, Mwenye kurehemu)) [Al-Hujuraat: 12]
Ibn 'Abbaas (Radhiya Allaahu 'anhuma) amesema: Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Ameharamisha Muumimi kumsengenya mwenziwe kama Alivyoharamisha nyamafu.
Maulamaa wamekubaliana kuwa Ghiybah ni haraam kama alivyonukuu Imaam An-Nawawy.
Kauli: 
(( فَكَرِهْتُمُوهُ ))
((Mnalichukia hilo))
kwa maana kama mnavyochukia kula nyama ya ndugu yenu aliyekufa basi vile vile mchukie kumtaja mwenzenu kwa ubaya.

Anasema pia Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala):
 ((وَلاَ تَلْمِزُوا أَنفُسَكُمْ وَلَا تَنَابَزُوا بِالْأَلْقَابِ بِئْسَ الاِسْمُ الْفُسُوقُ بَعْدَ الْإِيمَانِ وَمَن لَّمْ يَتُبْ فَأُوْلَئِكَ هُمُ الظَّالِمُونَ))
((Wala msitukanane kwa kabila wala msiitane kwa majina ya kejeli. Ni uovu kutumia jina baya baada ya kwisha amini. Na wasiotubu, hao ndio wenye kudhulumu)) [Al-Hujuraat: 11]

Mwenye kufanya hivyo; mwenye kusengenya na mwenye kumzushia mwenziwe uongo wamelaaniwa na kushutumiwa na Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) katika Aayah ifuatayo:
((وَيْلٌ لِّكُلِّ هُمَزَةٍ لُّمَزَةٍ))
((Ole wake kila safihi, msengenyaji!)) [Al-Humazah: 1]
Ibn 'Abbaas (Radhiya Allaahu 'anhuma) amesema: "Humazah ina maana yule anayetukana na kufedhehesha wenziwe" [At-Twabariy 24: 596] 
Al-Hammaaz:   Mwenye kusengenya kwa vitendo kwa mkono au kwa macho kama kukonyeza.  
Al-Lammaaz: Mwenye kusengenya kwa ulimi (kunena).
[Kauli ya Mujaahid katika Tafsiyr ya Ibn Kathiyr]

Yote hayo ni Ghiybah na adhabu zake ni kama tulivyosoma katika Aayah ya juu hapo; ni mfano wa kula nyama ya ndugu yako aliyekufa. Na pia ni kuonywa na Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) kwa 'wayl' ambayo maana yake ni:
1.     Neno la kutisha lenye maana ya kudhalilishwa, kuadhibiwa na kungamizwa.
2.     Ni bonde katika  moto wa  Jahannam

Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) kwa wanaosengenya kwa kuzulia watu maovu,
((إِنَّ الَّذِينَ يُحِبُّونَ أَن تَشِيعَ الْفَاحِشَةُ فِي الَّذِينَ آمَنُوا لَهُمْ عَذَابٌ أَلِيمٌ فِي الدُّنْيَا وَالْآخِرَةِ وَاللَّهُ يَعْلَمُ وَأَنتُمْ لَا تَعْلَمُونَ))  
((Kwa hakika wale wanaopenda uenee uchafu kwa walioamini, watapata adhabu iumizayo katika dunia na Akhera. Na Allaah Anajua na nyinyi hamjui)) [An-Nuur: 19].

No comments:

Post a Comment