Social Icons

rss feed facebook twitter google plus linkedin youtube email

Thursday, May 3, 2012

Waislam Tunapaswa Kubadilika Sasa.


Assalamu Alaikum Wa Rahmatu Allah Wa Barakatuh
Ndugu zangu katika imaan, mara nyingi nimekuwa nikisoma malalamiko mengi sana kutoka upande wetu sisi Waislam. Kiasi ambacho sasa imekuwa kama wimbo usiochezeka tena.

Kwanini nasema hivyo, nina sababu nyingi lakini hapa ninaweza kuelezea zile chache amabazo nitajaaliwa kuzieleza Insha’Allah.

Waislam leo inaonekana kama ni watu ambao wapo nyuma kimaendeleo, kimasomo na kwenye kila Nyanja za kimaisha, japokuwa kwa mtu mmoja mmoja inaonekana kama waislam tuna maendeleo makubwa, ili linaweza kuwa kweli kwa sababu mambo mengi ambayo sisi Waislam tunayafanya yanakuwa kama hayana Baraka kutoka kwa Mwenyezi Mungu, ukiudhuria mihadhara mingi ukosi kusikia malalamiko kutoka kwa waadhiri kuwa Waislam tunanyanyaswa na kuonewa, lakini hapo hapo tunashindwa kujiangalia sisi wenyewe Waislam, tumefanya nini au tunafanya jitihada gani katika kujikwamua katika matatizo haya na hapo hapo kufuata mafundisho ya dini yetu.
Wakati mwingine nahisi hii ni kama dalili za adhabu kwetu, maana Waislam tumekuwa hatuna tofauti na hao Wakristo, Wapagani na wale wasio amini kuwepo kwa Mwenyezi Mungu. Hizi rehma na riziki ambazo tunazipata mi nahisi ni kwa sababu kuna viumbe vingine ambavyo havina makosa, kama vile wanyama na mimea, kutokana na hao ndio na sisi tunafaidika.

Waislam ndio tunaongoza kwenye mambo mengi ya kipuuzi, utakuta waimbaji wazuri kwenye miziki ni waislam, kwenye uhuni wa kufuta bangi, madawa ya kulevya na ulevi mwingine, waislam tunaongoza, kiasi hata hao wakristo uwa wanatufanyia istizahi kuwa mbona mwezi wa ramadhani mabaa na maeneo yanauza nyama ya nguruwe (kiti moto) uwa yanakosa wateja na hayajazi kama miezi mingine. Mbona tunapomaliza mfungo ndio mabaa na majumba ya kufanyia ngono ndio yanafurika?
Si ajabu leo kumkuta Muislam akisema uongo ili apate pesa, kazi au biashara, leo hii Muislam yupo radhi kwenda kwenye shirki ili aweze kufanikiwa kwenye biashara zake. Waislam sisi tupo sawa na hao wasio amini kwenye makatazo mengi, leo hii sisi ndio matajiri na pesa zetu zipo kwenye mabenki yenye kutoa riba. Hatuwaangalii watoto yatima, kiasi tumewapa majina kama vile Machokoraa au watoto wa mitaani, mimi binafsi sijawahi kuona mitaa ikizaa watoto, lakini ndivyo tunavyo waita.

Matajiri wamekaa kwenye majumba yao wakila na kusaza na haya wanayajuwa na hata kuonyesha mfano wa kufungua kituo cha kulelea watoto ili kesho na kesho kutwa waje kuwa watu wema wanashindwa, hivi tutakuja kusema nini kesho tutakapo simama mbele ya Mwenyezi Mungu?

Waislam tunapaswa kubadilika, maana Mwenyezi Mungu awezi kubadilisha hali zetu mpaka sisi wenyewe tuchukue hatua za makusudi kabisa na kufanya jitihada za dhati ndipo naye Mwenyezi Mungu atatufungulia milango yake ya Rehma na Uislam utasimama tena.

Wakati wa kukaa vibarazani na kwenye mimbari na uku tukilaumu mfumo kristo, bila ya kuchukuwa hatua madhubuti za kupigania jihadi ya nafsi zetu, hazita tufikisha popote. Mfumo wowote m baya uondoka pale tu wahathirika wakuu watakapokuwa kweli wameamini ki kweli kweli na kuwa ni Waislam wa kweli na si Waislam kwa majina na mavazi tu. Wakati ndio huu, hatuja chelewa bado, turejee kwenye Uislam aliotuachia Mtume (s.a.w) na si kuhadaika na mifumo ya kidunia, mifumo ambayo inatutenga sisi Waislam.

Badala yake sisi wenyewe Waislam ndio tumekuwa watu wa mbele kuiendeleza nifumo hiyo ambayo leo inatuwacha nyuma. Sisi wenyewe ndio tunaondoa Uislam katika taaluma zetu. Sisi Waislam ndio wenye majumba ya ufuska; kama vile mabaa, vilabu vya usiku pamoja na kila kitu ambacho kipo nje ya itikadi na maadili.

Hali hii inapelekea athari za Qur`an na Sunna za Mtume kufichika katika maisha ya kijamii kama si kuhama kabisa. Hata lugha ambayo Qur’an ndio inaitumia yaani Kiarabu tunaitupa na ndio sisi hao hao tumekuwa mahodari katika kutoa fatwa mbali mbali.
Ndio maana kikawa kizazi hiki hakijishughulishi na dini wala maadili mema. Hiyo ni natija ya ufisadi wa nafsi zetu wenyewe maana watoto zetu tunawalea na wanakulia kwenye mitandao ya internet na video game.

Hakika tumeshafanya makosa na tunaendelea kufanya makosa, tunajitenga na tabia za Kiislam na tunarithisha mambo mabaya kwa kizazi chetu kwa maana ya watoto zetu. Hakika tunakitenga kizazi na Uislam. Hawakukosea wale waliosema: "mtoto umleavyo ndivyo akuavyo."

Wengi wanaweza kutaka kujuwa dawa yake ni nini kwa hali hii tulio nayo hivi sasa?
Kwa kweli jibu la swali hili si la kulijibu mimi, mimi ni kama mchokozi na mchokonoaji wa hoja, mambo haya yanataka wasomi na Masheikh waliobobea wenye akili kubwa zenye ikhlas. Wakae na kuamua nini cha kufanya na nini cha kutuambia sisi maamuma wao. Kwa kweli tunapaswa kula chakula cha roho, chakula ambacho kitaweza kurutubisha mioyo yetu na kumrejea Mwenyezi Mungu, maana yeye ni Mwingi wa rehma na Mwingi wa Msamaha, na Mwenyezi Mungu hashindwi kufanya Qur`an, sharia yake na maadili yake, kuwa ndiyo inayotawala leo.

Lakini ni juu yetu kufanya juhudi kadiri ya uwezo wetu, wala tusingoje muujiza wa mbinguni. Na kazi ambayo tunaweza kuifanya, nionavyo mimi, ni: kwanza, tuitilie mkazo elimu ya dini ya Kiislam katika mashule, hasa Qur`an, kuisoma, kuihifadhi na kuifasiri. Kwani hiyo ndiyo msingi. Basi ni juu yetu kuwapeleka watoto zetu kwenye mashule ya Kiislam na kufuatilia kile wanacho fundishwa na tukishindwa basi tuwapeleke madrasa, ili uko wapate kujifunza misingi ya dini yetu.

Pili, kila mmoja katika watu wa dini atekeleze wajibu wake kwa ikhlasi, na kujiandaa kuwa kiongozi mwenye mwamko, anayejua namna ya kuwakinaisha vijana kuwa dini ndio chimbuko la msimamo ulio sawa, ambalo litawapa maisha mema zaidi.
Tatu, kuufafanua uhakika wa dini, kuufanya mwepesi kufahamika na kuutangaza kwa kutumia vitabu, hotuba, Tovuti baraza, blog, makala na matoleo mbalimbali. Tumthibitishie mjinga na mwenye shaka kuwa Uislamu, kwa sharia na maadili yake, unatosheleza kabisa mahitaji ya mwanaadamu ya kiroho na ya kimaada; na unaweza kutatua matatizo yake; na kwamba una lengo la kumfanya afaulu katika dunia yake na akhera yake.

Kuzibadilisha nasfi zetu kunahitaji juhudi na jihadi ndefu, zenye kutuweka kwenye mitihani na majaribu mengi; kama juhudi aliyoifanya Mtume (s.a.w) katika kubadilisha ada za kijahiliya na itikadi zao. Mtume (s.a.w) anasema hivi: "Uislamu ulianza katika hali ya ugeni, na utarudi katika hali ya ugeni kama ulivyoanza."

Kwa hiyo, hatuwezi kuepukana na ugeni wake kwani Uislam ni mpana sana na tunatakiwa kufanya jitahada za makusudi kabisa kuambatana nao, ni wajibu wetu sisi wenyewe kuamua kwa dhati kabisa kuifanya Qur`an, ndio Mwongozo wetu na si kimaneno tu, hata tabia zetu ziendane kama tunavyo fundishwa kwenye Qur'an na Sunna. Maana tunafundihswa na Mtukufu wa darja kuwa, ukiona jambo baya liondowe kwa mkono wako, kama huwezi basi lisemee watu wasikie kama hili baya, Jambo la mwisho kama hayo yote uwezi basi angalau lichukie kwenye moyo wako na hili la kuchukia ni katika Imani dhaifu sana, na imani dhaifu ndio tuliokuwa nayo sisi Waislam leo.

Na kuna kauli moja inasema hivi, dalili za mtu mnafiki ni tatu, anaposema anaongopa, anapotoa ahadi hatimizi/anaivunja, anapoaminiwa na amana hufanya khiyana. Na dalili zote hizo zipo kwa Waislam sisi.

Tunashindwa kuondoa ufisadi na kwenye nafsi zetu, kwenye majumba yetu, kwenye biashara zetu, ili hali haya yote yapo ndani ya uwezo wetu, tunacho kijuwa sisi ni kulalamika ili hali haya yote tunayatengeneza sisi wenyewe

No comments:

Post a Comment