Social Icons

rss feed facebook twitter google plus linkedin youtube email

Tuesday, July 24, 2012



                Abdallah Bin Eifan
            (Jeddah, Saudi Arabia)

Alhamdullaah nashukuru, namshukuru Qudusi,
Kutwa tunamdhukuru, kwa wingi bila kiasi,
Apate kutunusuru, na adui ibilisi,
Ramadhani Imefika, Mungu Tusamehe Dhambi.

Hili ni Kumi la kwanza, litapita kwa upesi,
Sote  tunabembeleza, rehema Zake Mkwasi,
Dua tumeziongeza, Tunamuomba halisi,
Ramadhani imefika, Mungu Tusamehe Dhambi.

Tusije tukateleza, kuyarudia maasi,
Mungu Atatuongoza, Atutoe wasiwasi,
Mungu Atupe Mwangaza, tuone kwa urahisi,
Ramadhani Imefika, Mungu Tusamehe Dhambi.

Walokufa Warehemu, peponi Wape nafasi,
kaburini Wakirimu, upweke wasiuhisi,
Wewe Mola ni Adhimu, kwa Kusamehe Mwepesi,
Ramadhan Imefika, Mungu Tusamehe Dhambi.

Mungu ondoa magonjwa, khasa ule wa ukimwi,
Watoto kuambukizwa, kosa lao hawajuwi,
Mayatima wamekuwa, na tena hawaulizwi,
Ramadhani imefika, Mungu Tusamehe Dhambi.

Mungu ondoa ukame, Waokoe wakulima,
Mvua Usiwanyime, mazao yatasimama,
Dua zote tuzisome, leo, kesho na daima,
Ramadhani imefika, Mungu Tusamehe Dhambi.

Waongoze wasichana, wapate kujifunika,
Hijaab ni kinga sana, wapate kusitirika,
Ni vazi lenye heshima, tena limewajibika,
Ramadhani imefika, Mungu Tusamehe Dhambi.

Waongoze wavulana, wapate kunusurika,
Uhuni kuepukana, tabia kubadilika,
Waongoze Subhaana, dini yao kuishika,
Ramadhani imefika, Mungu Tusamehe Dhambi.


Mungu Walipe vipofu, Uwaingize peponi,
Bubu awe kwenye safu, na kiziwi masikini,
Wamesubiri pungufu, na shida zote mwilini,
Ramadhani imefika, Mungu Tusamehe Dhambi.

Mtukufu huu mwezi, viumbe tuwe azizi,
Ni mwezi wenye malezi, na mwezi wa mazoezi,
Huku tukifanya kazi, na ibada tuienzi,
Ramadhani imefika, Mungu Tusamehe Dhambi.

Tusamehe Mola wetu, sisi viumbe dhaifu,
Tufutie dhambi zetu, Tunakuomba Raufu,
Tusafishe kila kitu, tusibakize uchafu,
Ramadhani imefika, Mungu Tusamehe Dhambi.

Wakati unakupita, unakimbia kwa kasi,
Wakati utakukata, kama kanga na mkasi,
Omba sana utapata, tulia na ujilisi,
Ramadhani Imefika, Mungu Tusamehe Dhambi.

Mungu Anapenda sana, Anaemuomba sana,
Kwa hivyo tuombe sana, ili Atupende sana,
Akishatupenda sana, Atatupa nyingi sana,
Ramadhani imefika, Mungu Tusamehe Dhambi.

Hitimisha Qur-ani, ni mwezi uloteremshwa,
Uende msikitini, tarawih ikiswalishwa,
Qiyaamul-Llayl swalini, kama tulivyofundishwa,
Ramadhani imefika, Mungu Tusamehe Dhambi.

Fanyeni mambo ya kheri, anza ndugu na jirani,
Toa sadaka kwa siri, usitaje asilani,
Ghadhabu Zake Qahari, zinapozwa kwa yakini,
Ramadhani imefika, Mungu Tusamehe Dhambi.

Jitolee kwa futari, peleka msikitini,
Apate kula fakiri, pamoja na masikini,
Au katoka safari, mlishe huyo mgeni,
Ramadhani imefika, Mungu Tusamehe Dhambi.

Uwaombe msamaha, wale ulowakosea,
Hapo utahisi raha, deni umeshalipia,
Epukana na karaha, viumbe kuwaonea,
Ramadhani imefika, Mungu Tusamehe Dhambi.

Mtu akikutukana, usimjibu nyamaza,
Ukianza kugombana, saumu utapoteza,
Ni mwezi wa kupatana, subira kutekeleza,
Ramadhani imefika, Mungu Tusamehe Dhambi.

Mola wetu na Muumba, Pokea zetu amali,
Radhi Zako tunaomba, dua zetu Zikubali,
Sote tumeshika kamba, tunaomba tunaswali,
Ramadhani Imefika, Mungu Tusamehe Dhambi.

Nafunga shairi langu, tutazidi kuonana,
Nisameheni wenzangu, kama tumekoseana,
Atatusamehe Mungu, ikiwa tumeshikana
Ramadhani Imefika, Mungu Tusamehe Dhambi.

No comments:

Post a Comment