Social Icons

rss feed facebook twitter google plus linkedin youtube email

Thursday, July 12, 2012

fadhila za mwezi wa ramadhani

Ama kwa hakika katika mwezi wa Ramadhaan kuna fadhila nyingi ambazo mimi nitazitaja kwa uchache namuomba Allaah Aniwafiqishe 'asaa yawe na manufaa katika Duniya na Akhera Insha-Allaahu  Aamiyn.
 
1)     NI MWEZI WA QUR-AAN: 
Kama Alivyosema  Mwenyeezi Mungu Mtukufu katika kitabu Chake:
"Mwezi wa Ramadhaan ni mwezi ambao imeteremshwa Qur-aan ili iwe uongozi kwa watu na hoja na upambanuzi (Baina ya haki na batil)”Qur-aan 2:185
Na imekua makusudio yake  ni kuteremshwa Qur-aan kutoka katika Lawhum-Mahfuudh ilaa samaai dduniya (Kutoka Lawhim-Mahfuudh mpaka mbingu ya kwanza). 
Vilevile kama ilivyopokewa na Ibn 'Abbaas (radhiya Allaahu 'anhu) kuwa  makusudiyo yake   kwa hakika kuteremshiwa Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa sallam) Qur-aan mwanzo ni katika mwezi wa Ramadhaan na vilevile Qur-aan mwanzo wa kuteremka ni usiku wa Laylatul-Qadir na Laylatul-Qadir iko katika mwezi wa Ramadhaan.
Hivyo basi ni juu yetu kufanya juhudi katika mwezi huu kukithirisha sana kusoma Qur-aan.  Walikua Salafus-Swaalih (Wema Waliotangulia) wakikilinda kitabu cha Allaah kwa kukisoma na kuyafanyia kazi yaliyokuwemo kwa mazingatiyo. Pia Tunaambiwa kuwa Sayyidnaa Jibriyl (‘Alayhis-Salaam) akimfundisha Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa sallam) Qur-aan katika mwezi wa Ramadhaan, na alikuwa 'Uthmaan bin 'Afaan (Radhiya Allaahu 'anhu)  kila siku akisoma Qur-aan yote yaani anakhitimisha mara moja kwa siku,  kwa maana,  msahafu mzima anausoma kwa siku moja. Na walikuwa baadhi yao katika wema wakisoma Qur-aan yote kwa siku tatu, wengine kwa wiki moja na wengine kwa siku kumi. Walikuwa wakisoma Qur-aan ndani ya Swalah na nje ya Swalah.
Mwenyeezi Mungu Atuwafiqishe mimi na wewe tuisome Qur-aan na kwa mazingatiyo khasa katika mwezi huu tufanye juhudi sana ili tuweze kupata fadhila za mwezi huu mtukufu.
 
2)     NI MWEZI WA SUBIRA:
Subira ni katika jambo gumu na halipati ila kwa mtu mcha Mungu na mnyenyekevu kwa Allaah. Na katika kufunga kunatakiwa subira pale mtu anapojizuilia kutokana na kutokula, kunywa, matamanio na mengineyo. na imekua Swawm ni nusu ya subira na subira malipo yake ni pepo kama alivyosema Mwenyeezi Mungu Mtukufu:
"Kwa hakika (Mwenyeezi Mungu) Atawapa wenye kusubiri malipo bila ya hisabu"Qur-aan 39:10:
 
3) MILANGO YA MOTO INAFUNGWA, MILANGO YA PEPO INAFUNGULIWA NA MASHETANI WANAFUNGWA:
Kama ilivyokuja katika Hadiyth iliyopokelewa na Maimamu wawili:
Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa sallam) amesema, "Pindi inapokuja Ramadhaan inafunguliwa milango ya pepo, na hufungwa milango ya moto, na mashetani wanafungwa kwa Minyororo" (imesimuliwa na Al-Bukhaariy na Muslim)
Kwa hakika utaona katika mwezi huu watu wengi wanajitahidi kujiepusha na maasi, watu wanajaa misikitini kwa kufanya ibada ya mwezi huu hii ni kwa sababu mashetani wamefungwa na shetani juu ya uasi wake lakini anauogopa mwezi wa Ramadhaan na vitimbi vyake vinakuwa dhaifu ndio mana wengi nyoyo zinabadilika wanaswali  na kujitahidi kufanya kheri.  Lakini ikimalizika Ramadhaan tu basi Swalah imekwisha kama vile Allaah yupo Ramadhaan tu. Huu ni msiba ndugu zangu Waislamu Allaah Asitujaalie katika hao.
 
4)     LAYLATUL QADR:
Katika mwezi huu kuna siku ya Laylatul-Qadr siku ambayo ni bora kuliko miezi elfu kama  Alivyosema Mwenyeezi Mungu:
"Huo ni usiku wa hishima ni bora kuliko miezi elfu.
 Huteremka Malaika na roho (za viumbe watakatifu) katika (usiku) huo  
  kwa idhini ya Mola kwa kila jambo.
 Ni amani (usiku) huo mpaka mapambazuko ya alfajiri"
Qur-aan 97:3-5
Imehisabiwa mtu atakapofanya ibada katika usiku huo mmoja ni kama amefanya ibada sawa na miaka 83 na hii ni katika fadhila kubwa kabisa. Na katika kitabu Muwatwaa, Imamu Maalik  amesema.
Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa sallam) ameona umri wa umma za mwanzo ni mrefu, na umri wa ummah wake ni mfupi akapewa usiku wa Laylatul-Qadr uwe ni bora kuliko miezi elfu.
(Muwatwaa1/321 (Muhammad Fuad 'Abdul-Baaqy)
Hakuna siku tukufu na kubwa kama siku hii ni wajibu kwetu kuutafuta usiku huu katika kumi la mwisho kufanya ibada ili tupate fadhila hizo.  Ninamuomba Allaah atuwezeshe kwa hilo, AAMIYN.
 
5)     DU'AA NI ZENYE KUKUBALIWA:
Katika hadiyth iliyopokewa na Imaam Ahmad:
Kutoka kwa Jaabir (radhiya Allaahu 'anhu) kwa isnadi iliyo nzuri
Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa sallam) Amesema: "Kila Muislam du'aa zake ni zenye kukubaliwa atapomuomba katika mwezi wa Ramadhaan"
Na imepokewa katika Hadiyth kuwa du'aa ya mwenye kufunga pia ni yenye kukubaliwa. Basi mtu ajipinde katika kumuelekea Allaah kumuomba mambo ya kheri ya dunia na akhera aombe pepo ya Jannaatul Firdaus na alete maombi mengine Insha Allaah Mwenyeezi Mungu Atayapokea maombi yetu, AAMIYN.
 
La mwisho ambalo nitakua nimekamilisha maudhui yangu:
 
6) MWEZI HUU NI MWEZI WA KUTOA:
Na alikua Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa sallam) akizidisha kheri nyingi katika mwezi wa Ramadhaan.
Imepokewa na At-Tirmidhiy kutoka kwa Anas (Radhiya Allaahu 'anhu) Kasema Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa sallam) "Bora ya (wakati wa) kutoa sadaqa ni kutoa katika mwezi wa Ramadhaan"
Na imepokewa na Zayd bin Aslam kutoka kwa babake, amesema nimemsikia 'Umar bin Al-Khattwaab (Radhiya Allaahu 'anhu) anasema, "Ametuamrisha Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa sallam) tutoe sadaqa nikatoa mali yangu nikasema leo nimemtangulia Abu Bakr nimekwenda na nusu ya mali, akasema Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa sallam) kuniambia, "Umewabakishia nini watu wako?" Nikasema, nusu kama hii, na akaja Abu Bakr na kila mali yake Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa sallam) akamuuliza, "Umewabakishia nini watu wako?Akasema, nimewabakishia Mwenyeezi Mungu na Mtume wake. Nikasema huyu Abu Bakr hapitiki na kitu chochote abadan"
Kuonyesha wema waliotangulia walikua wakishindana katika kheri lakini tofauti kubwa katika zama zetu hizi watu wanashindana katika mambo ya kidunia na kujifakharisha nayo. 
Tunamuomba Allaah Atuonyeshe mema tuyafuate na mabaya tuyawache na tushindane katika kila kheri ili tuwe ni wenye kufuzu na kupata daraja ya juu ya Pepo.

No comments:

Post a Comment