Social Icons

rss feed facebook twitter google plus linkedin youtube email

Tuesday, July 17, 2012

UKHALIFA WA SAYYIDNA ALIY BIN ABI TWAALIB (35 – 40 H.)

Baada ya kuuawa kwa khalifa aliye dhulumiwa, Waislamu wakawa wamedangana/wamehemewa, hawana wa kumkimbilia, likawa zogo/vurugu/fujo. Na hawakuwa na mtu anaye stahiki kuwa khalifa baada ya Sayyidna Uthman ila Sayyidna Aliy bin Abi Twaalib. Basi wengi wao wakamuendea kumtaka autawalie ukhalifa. Naye akauangalia mustakabali wa hali ya Waislamu kwa umakini mkubwa na akatambua ya kwamba anakabiliwa na fitina itembeayo, isiyo wezwa kuzuiwa. Akawaambia: Mtafuteni mtu mwingine, kwani hakika sisi tumekabiliwa na jambo ambalo lina uwepo wake na lina rangi kadhaa, nyoyo haziliwezi na wala akili hazithibiti juu yake. Basi wakamuomba na kumsihi kwa ajili ya Allah na dini yake. Akawaambia: Nimekuitikieni (nimeyakubali maombi yenu). Na jueni ya kwamba nikikuitikieni, nitakupandisheni garI ninalo lijua (nitakuongozeni kwa sera zangu). Na mkiniacha (msinipe uongozi), basi hakika si vinginevyo mimi ni sawa na yeyote katika nyinyi, ila tu mimi ni mtii na msikivu mno kwa mtakaye mtawadha ukhalifa. Nao hawakumkubali ila yeye tu.
Kisha wakaona ya kwamba suala hili haliwezi kutimia ila kwa ulaji kiapo cha usikivu na utii cha Zubeir bin Al-Awaaam na Twalhah bin Abdillah. Basi likatoka kundi kuwaendea, wakaja nao wakala kiapo cha utii na usikivu kwa khalifa. Katika mapokezi mengine yasemekana waliletwa kwa nguvu. Na yasemekana kwamba Zubeir hakula kiapo aslan. Halafu ndio na watu wengine wakainuka, wakaenda kula kiapo cha utii na usikivu kwa khalifa. Na likabakia nyuma lisile kiapo kwa khalifa, kundi katika maswahaba wakubwa wa Madina, kama Sa’ad bin Abi Waqaasw, Said bin Zaid, Abdullah bin Umar. Usaamah bin Zaid, Al-Mugheerah bin Shu’ubah, Abdullah bin Salaam, Qudaamah bin Madhw-oun, Abu Said Al-Khudriy, Ka’ab bin Ujrah, Ka’ab bin Maalik. Noumaan bin Bashir, Hassaan bin Thaabit, Maslamah bin Mukhallad, Fudhwaalah bin Ubeid na wengineo katika maswahaba wakubwa wa miji mingine. [MUQADDIMAH BIN KHALDOUN]
Sayyidna Aliy-Allah amuwiye radhi-alipo ona kwamba zoezi la kula kiapo cha utii na usikivu kwake kama khalifa wa nne wa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-limekamilika. Akainuka na kuwakhutubia watu, akamuhimidi na kumsifia Allah, kisha akasema: (Enyi watu! Hakika Allah ameteremsha kitabu ambacho ni chenye kuongoza, anabainisha humo kheri na shari, basi kheri ifuateni na shari iacheni. Yaliyo ya faradhi yatekelezeni kwa Allah Ataadhamiaye, hilo litakupelekeeni (kuingia) peponi. Hakika Allah ameyatukuza matukufu mengi ambayo si yenye kufichikana na akaufadhilisha utukufu wa muislamu juu ya yote yaliyo matukufu. Na akazifunga haki za Waislamu kwa Ikhlaasi na Tauhid. Kwa hivyo basi, muislamu wa kweli ni yule ambaye waislamu (wenzake) wamesalimika kutokana na (shari ya) ulimi wake na mkono wake, ila kwa haki. Na si halali (kumwaga) damu ya mtu muislamu ila kwa yale yanayo wajibisha (kumwagwa). Yatangulizeni mbele mambo ya umma khususan anapo fikwa na mauti mmoja wenu. Kwani hakika watu wako mbele yenu na hakika si vinginevyo kilichoko nyuma yenu ni saa (Kiyama). Ipunguzeni mizigo ya madhambi, mtafika salama (Akhera), kwani hakika si vinginevyo watu wanangojewa na Akhera yao. Enyi waja wa Allah! Mcheni Allah katika mji wake na kwa waja wake, bila ya shaka nyinyi mtaulizwa hata kuhusiana na vipande vya ardhi na wanyama. Mtiini Allah na wala msimuasi. Na mtakapo iona kheri, basi iandameni na mtakapo iona shari, basi iepukeni. “NA KUMBUKENI MLIPO KUWA WACHACHE, MKIONEKANA WANYONGE KATIKA NCHI...”. [08:26]
Kisha akashuka kutoka mimbarini. [TAARIKHUT-TWABARIY 02/698]

  1. Wasifu wa Sayyidna Aliy:
Khalifa huyu wa nne wa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-yeye ni Aliy bin Abi Twaalib, bin Abdil-Mutwalib, bin Hashim, mkuraishi wa ukoo wa Hashim, binamu wa Mtume wa Allah. Na mama yake ni Bi. Fatmah bint Asad, bin Hashim, bin Abdi Manaaf. [AL-ISWAABAH 04/564, AT-TWABAQAAT AL-KUBRAA 02/259, TAARIKHU KHALIFAH BIN KHAYYAATW, sah. 80 & TAARIKHUT-TWABARIY 01/537].
Alizaliwa Imamu Aliy-Allah amuwiye radhi-mnamo mwaka wa thelathini na mbili, tangu kuzaliwa kwa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie. Wakati Mtume anakabidhiwa na Mola wake majukumu mazito ya utume, Sayyidna Aliy alikuwa chini ya umri wa baleghe. Na alikuwa akisakini (akiishi) pamoja na Mtume katika nyumba yake (Mtume), akimlisha na kunywesha kwa sababu ya ufakiri ulio mkumba baba yake (Mzee Abu Twalib; ami yake Mtume). Kwa ajili hiyo (ya kulelewa katika nyumba ya Mtume), akaongoka na muongozo wa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie. Na wala hakujiboronga na uchafu/najisi ya jaahiliya, yaani hakupata kuyaabudu masanamu na maovu mengine yaliyo kuwa yakitendwa katika zama hizo za viza vya jaahiliya.
Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alipo gura (hama) kutoka Makka kwenda Madina, Imamu Aliy alimfidia kwa kuitoa muhanga nafsi yake. Pale alipo lala kwenye kirago chake, tena akajifunika shuka lake, ili wale walio izingira nyumba ya Mtume, waendelee kudhania ya kwamba Mtume angali amelala, ili wasimpe taabu katika kutoka kwake. Baada ya fidaa hiyo, naye huyoo akaondoka Makka kwenda Madina kuungana na Mtume wa Allah huko.
Sayyidna Aliy-Allah amuwiye radhi-alibahatika kushiriki pamoja na Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-katika vita vyake vyote, ila vita vya Tabuuk. Hakwenda katika vita hivyo, kwa kuwa Mtume alimkaimisha ukhalifa wa Ahali beit wake na akamwambia: “Hivyo wewe huridhii kuwa kwangu kama daraja aliyo kuwa nayo Harun kwa Musa, ila tu ni kwamba hapana utume baada yangu”. Bukhaariy [3706, 3503] & Muslim [2404]-Allah awarehemu.
Imamu Aliy-Allah amuwiye radhi-alikuwa na mchango mkubwa katika vita vyote, naye ndiye mtu wa kwanza kufanya mubaaraza (mpambano wa watu wawili) katika vita vya Badri. Naye ni miongoni mwa wale watu walio thibiti katika medani, katika vita vya Uhud na Hunein wakati ambao maswahaba walichangukana kutokana na ukali wa mashambulizi ya adui, wakamuacha Mtume na maswahaba wachache walio thibiti pamoja nae. Na kwa mikono (juhudi) yake, ilifunguliwa ngome madhubuti ya Mayahudi, Khaibar.
Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-alimuoza Imamu Aliy, binti yake Faatimah, mnamo mwaka wa pili wa Hijra. Bibi Faatimah akamzalia Imamu Aliy watoto; Hassan, Hussein, Zainab al-kubraa na Ummu Kulthum al-kubraa.
Imamu Aliy-Allah amuwiye radhi-alizisoma kwa niaba ya Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-aya za mwanzo za Surat Tauba, katika msimu wa Hijja. Kwa ajili ya kutangaza kutupiliwa mbali dhima ya Allah na Mtume wake, kwa washirikina.
Alipo fariki Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie-na Sayyidna Abubakar akachaguliwa kuwa khalifa wake, Imamu Aliy-Allah amuwiye radhi-naye alimpa baia (kiapo cha utii na usikivu) pamoja na kwamba alikuwa akiona kuwa yeye ndiye mstahiki wa ukhalifa, kwa sababu ya udugu wake kwa Mtume wa Allah-Rehema na Amani zimshukie. Lakini ni kwamba yeye alikuwa akiichukia khilafu (kukhitalifiana na kuzozana). Ni kwa ajili hiyo ndio Muhammad bin Siiriin; taabii akazikadhibisha kauli zote zilizo nasibishwa kwa Imamu Aliy, kauli ambazo ndani yake kuna kupomosha (kuangusha) makamo (daraja) ya masheikh wawili; Abubakar na Umar-Allah awawiye radhi. Kama yalivyo pokewa hayo katika SAHIH AL-BUKHAARIY.
Na ukhalifa ulipo twaliwa na Sayyidna Umar-Allah amuwiye radhi-kadhaalika alimpa baia, pamoja na hivyo akamuoza binti yake; Ummu Kulthum. Na ni mara nyingi tu Sayyidna Umar alikuwa akimkaimisha uongozi wa Madina pale anapo toka nje ya Madina. Na hata Sayyidna Uthman-Allah amuwiye radhi-alipo tawazwa kuwa khalifa wa Waislamu baada ya Sayyidna Umar. Kadhaalika alimpa baia mpaka mwisho wa ukhalifa wake walipo simama dhidi yake wale waasi na wakamtia dosari kwa kuwapa madaraka ndugu zake. Na ni mara nyingi tu, Sayyidna Aliy alikuwa akimpa kwa moyo mkunjufu nasaha na akimuongoza kwenye yale ambayo ndani yake kumo kufaulu kwa umma. Lilipo timia lililo hukumiwa na Allah na Sayyidna Uthman akauawa shahidi, Waislamu walimuendea Sayyidna Aliy na wakampa baia ya ukhalifa, mwezi 25, Dhul-Hijja, mwaka 35H. Akalibeba jukumu zito la ukhalifa, katika kipindi cha mzozo na vurugu baina ya Waislamu, kwa kipindi kinacho karibia miaka mitano ambamo haimkumtakatia hata siku moja. Na amri ya Allah ni kudra iliyo kwisha kadiriwa.

Imamu Aliy-Allah amuwiye radhi-alikuwa na rangi ya maji ya kunde, mwenye macho makubwa, kitambi na upara. Mwingi wa ndevu na nywele za kifua. Si mrefu wala si mfupi wa kuchusha, mwenye mikono na miguu yenye nguvu. Alikuwa mzuri wa sura, mwingi wa tabasamu.
Sayyidna Aliy-Allah amuwiye radhi-mbali na watoto wake alio zaa na Bibi Faatimah bint Rasuuli, alijaaliwa kupata watoto wengine kwa wake zake wengine. Watoto hao ni: Abbas, Ja’afar, Abdullah, Uthman, Ubeidillah, Abubakar, Muhammad Al-Asghar (mdogo), Yahya na Umar. Wengine ni Rukia, Muhammad Al-Ausatw (wa kati), Muhammad Al-Akbar (mkubwa) aliye tangaa kwa jina la Ibn Al-Hanafiyyah. Pia walikuwepo Hasan, Ramlah al-kubraa (mkubwa), Ummu Kulthum As-sughraa (mdogo), Ummu Haaniy, Maimunah, Zainab As-sughraa (mdogo) na Ramlah As-sughraa (mdogo). Watoto wake wengine ni: Faatimah, Umaamah, Khadija, Ummul-Kiraam, Ummu Salamah, Ummu Ja’afar, Jumaanah na Nafiisah. [AT-TWABAQAAT AL-KUBRAA 01/108, TAARIKHUT-TWABARIY 02/492 & AL-BIDAAYAH WAN-NIHAAYAH 07/366].

No comments:

Post a Comment