Social Icons

rss feed facebook twitter google plus linkedin youtube email

Saturday, August 17, 2013

MBIVU NA MBICHI KUHUSU HATMA YA SHEKH PONDA KUFAHAMIKA KESHO


Jumuiya na Taasisi za Kiislamu Tanzania, imetangaza mkutano wa dharura wa Waislamu jijini Dar es Salaam utakaofanyika kesho, kutafakari hatua za kuchukua kuhusu suala la Katibu wake, Sheikh Issa Ponda.
Hatua hiyo imefikia huku Jumuiya hiyo ikivilaumu vyombo vya usalama, kumuondoa Sheikh Ponda kutoka Taasisi ya Mifupa na Magonjwa ya Fahamu (Moi), akiwa hajamaliza matibabu na kumpeleka gerezani.
Aidha, jumuiya hiyo imelaumu taarifa za gazeti moja (siyo NIPASHE), kwamba Waislamu walipanga kuandamana jana, na kusema zililenga kuwachonganisha (Waislamu) na serikali.
Msemaji wa Jumuiya hiyo, Sheikh Rajab Katimba, akitoa tamko hilo kwa waandishi wa habari jana kwenye msikiti wa Mtambani jijini Dar es Salaam.
“Tunaalani kitendo cha polisi na usalama wa taifa, kutenda vitendo vinavyoashiria uonevu kwa viongozi wa dini ya kiislam, serikali itenda uadilifu kwa raia wake hata pale inapokuwa inaamini kuwa raia hao wana makosa,” alisema.
Alisema Jumuiya hiyo inashindwa kuamini kama mambo hayo yanaweza kufanywa na serikali, inayodai kutawala kwa kufuata utawala bora unaojali sheria, uadilifu, utu na uhuru wa kujieleza.
Alisema Jumuiya haikatai Sheikh Ponda kufunguliwa mashtaka lakini atendewe haki.
“Kitendo cha kumpiga risasi Sheikh Ponda na kisha kumtoa hospitalini na kumpeleka gerezani kwa kukiuka taratibu ni kinyume cha haki za binadamu, utawala bora na uhuru wa maisha ya mtu,” alisema Sheikh Katimba.
Sheikh Katimba ambaye alikuwa akisoma taarifa iliyosainiwa na Mwenyekiti wa Jumuiya hiyo, Sheikh Juma Said Ally, alisema Ponda anastahili haki ya matibabu hata kama anatuhumiwa.
Pia, alisema ufumbuzi wa suala la amani ya kweli na ya kudumu nchini ipo katika kushughulikia madai ya msingi ya Waislamu dhidi ya serikali, akisema ndiyo chanzo cha Sheikh Ponda, kupigwa risasi.
Sheikh Katimba, mkutano wa kesho utafanyika katika viwanja vya Nurul Yakin saa 9:00 alasiri, ambapo watatafakari na hatimaye kuchukua hatua za msingi zitakazoleta tija ya kweli ili viongozi wa kiislamu wasiendelee kudhalilishwa.
Naye Amiri Mkuu wa Baraza Kuu la Jumuiya na Taasisi za Kiislamu, Sheikh Mussa Kundecha, alisema Waislamu hawana mpango wa kufanya maandamano kama ilivyoripotiwa na baadhi ya vyombo vya habari.
Juzi, Sheikh Ponda, aliondolewa MOI alikokuwa akipata matibabu kufuatia kujeruhiwa mkoani Morogoro, ikiwa ni siku moja baada ya kusomewa mashtaka ya uchochezi akiwa kitandani.
Akizungumza na NIPASHE juzi muda mfupi baada ya tukio hilo, mke wa Sheikh Ponda, Khadija Ahmad, alisema saa 4:00 asubuhi, aliingia daktari ambaye hajawahi kumuona kwa kuwa siye aliyekuwa akimtibu mumewe.
Alisema daktari huyo alimwangalia mumewe kwa muda mfupi kisha akawaeleza kuwa mgonjwa anaendelea vizuri, hivyo ameamua kumruhusu.
Kwa mujibu wa Khadija, walipinga jambo hilo kwa kuwa hali ya mumewe waliona kuwa ilikuwa bado haijatengamaa.
Hata hivyo, alisema daktari huyo alishikilia msimamo wake na kutoka nje ya chumba alicholazwa Sheikh Ponda.
Alisema baada ya muda mfupi, waliingia askari kanzu wengi na kumchukua Sheikh Ponda bila kusema wanakompeleka. 
 
SOURCE::: NIPASHE

No comments:

Post a Comment