Social Icons

rss feed facebook twitter google plus linkedin youtube email

Tuesday, August 7, 2012

Waislamu Arusha wapinga uteuzi wa Kadhi Mkuu



WAISLAMU mkoani Arusha wamepinga uteuzi wa Kadhi Mkuu na Makadhi wengine wa mikoa 14 uliofanywa na Sheikh Mkuu wa Tanzania, Mufti Shaaban Simba kwa madai kuwa uteuzi huo ni wake binafsi na unalenga kuwavuruga waislamu nchini.
Hivi karibuni Mufti Simba alimtangaza Sheikh Abdallah Mnyasi kuwa Kadhi Mkuu na kuwateua Manaibu wake wawili, Sheikh Abubakar Zubeir na Sheikh Muhidini Mkoyogole.
Akipinga uteuzi huo, Imamu wa msikiti mkuu mkoani Arusha, Mohammed Hambal alisema kwamba uteuzi huo una makosa makubwa kwa kuwa Kadhi Mkuu huteuliwa na jopo la wasomi na sio mtu mmoja.
Alihoji kwamba taifa liko kwenye hatua ya uundwaji wa mchakato wa katiba mpya kwa sasa na kilio cha waislamu nchini ni uundwaji wa mahakama ya kadhi iingizwe kwenye katiba hiyo na kushangaa uteuzi huo kufanyika wakati huu.
“Wakati tume ya kukusanya maoni ikipita tunashangaa Mufti anamteua Kadhi Mkuu kitu ambacho ni kinyume na taratibu na mwogozo wa nchi,” alisema Hambal.
Hata hivyo, Hambal alihoji uteuzi huo umezingatia katiba ipi kwa kuwa katiba ya nchi pamoja na katiba ya BAKWATA haina kipengere wala maelekezo ya mfumo wa uundwaji wa mahakama ya kadhi.
Naye, Mwenyekti wa msikiti huo, Abdulazizi Mkindi alisema kwamba amepokea uteuzi wa Mufti kwa masikitiko makubwa kwa kuwa uteuzi huo umefanywa na kikundi cha watu wachache kwa lengo la kuwaongoza wailsamu nchini na taasisi zao.
Alisema kwamba masuala ya uteuzi wa Kadhi Mkuu yanapaswa kusimamiwa na watalaamu na wasomi waliobobea katika sheria na sharia za kiislamu na si vinginevyo.
“Kilio cha mahakama ya kadhi ni kilio cha wailsamu wote na si kilio cha BAKWATA pekee,masuala ya Kadhi yanatakiwa yasimamiwe na wataalamu waliosomea sheria na sharia za kiislamu na si watu wa ovyo,” alisema Mkindi.
Mustapha Kihago na Salim Mvungi maarufu kama Shefu kwa upande wao walipinga uteuzi huo na kusema kwamba wameshutushwa na wanahisi kwamba hizo ni njama za serikali kuitumia taasisi ya BAKWATA kuwavuruga wasilamu.
Walimnyooshea vidole Mufti Simba kuwa amelifanya suala la uteuzi wa Kadhi Mkuu kama ajenda yake binafsi wakati jambo hilo ni la wailsamu wote nchini.

No comments:

Post a Comment