Social Icons

rss feed facebook twitter google plus linkedin youtube email

Sunday, August 26, 2012

ZECO Pemba yatumia 29m/= kununua transfoma, nguzo




Mafundi wa Shirika la Umeme Zanzibar (ZECO) tawi la Pemba wakiwa katika harakati za kuwafungia transfoma wananchi wa kijiji cha Kichaka Shehia ya Mtangani Jimbo laKiwani Wilaya ya Mkoani Pemba , ambapo transfoma hiyo pamoja na nguzo 25 zimesgharimu zaidi ya shilingi 39 milion ambapo ni mchango wa wananchi zaidi ya shilingi 18 milion (picha na Haji Nassor, Pemba)

Na Haji Nassor, Pemba
ZAIDI ya shilingi 39 milion, zimetumiwa na Shirika la Umeme Zanzibar (ZECO) Tawi la Pemba, kwa ajili ya ununuzi wa trasfoma na nguzo 25, ambapo tayari jana trasfoma hiyo, imeshafungwa katika kijiji cha Kichaka Jimbo la Kiwani Wilaya ya Mkoani Pemba.
Kati ya fedha hizo zaidi ya shilingi 18 milion, ni mchango wa wananchi na shilingi 20 milion na laki nane, zimetolewa na ZECO ili kukamilisha upatikanaji wa huduma ya umeme kwa wananchi zaidi ya 1000 wa eneo hilo.
Akizungumza mara baada ya kazi ya ufungaji wa transfoma hiyo, huko Kichaka Msaidizi Afisa Uhusiano wa ZECO Tawi la Pemba Faki Othuman Sharif, alisema kuwa shirika kwa sasa limekuwa na utamaduni wa kusaidiana gharama na wananchi, iwapo wanahitaji kuwekewa transfoma.

Faki alieleza kuwa, hilo linatokana na shirika kujipanga upya kwa sasa, ili kuwaletea huduma bora wananchi kwenye sekta ya umeme, katika miji na vijiji mbali mbali ili uweze kuwasaidia katika kuinua kipato chao.
Afisa huyo aliwaambia wanavijiji vya Kichaka juu, Kinyasini, Utaani, pamona na Nga’ambu kuhakikisha wanajiungia umeme kwa lengo la kujinasua na umasikini uliokithiri miongoni mwa jamii za kizanzibari.
‘’Leo tumekamilisha ile kiu yenu ya miaka zaidi ya 20 mliokuwa nayo ya kutaka huduma ya umeme, na leo tayari tumeshafunga transfoma mpya kwa kushirikiana na nyinyi, hivyo huduma hii iwe kwa ajili ya maendeleo yenu’’,alifafanua .
Katika hatua nyengine Msaidizi huyo Afisa Uhusiano wa ZECO Tawi la Pemba amewahakikisha wananchi wa vijiji hivyo kuwa, kabla ya wiki tatu shirika la umeme litasambaaza waya mdogo, ili kutoa fursa kwa wananchi kuvuta majumbani mwao.
Mapema wakizungumza na mwandishi wa habari hizi, mara baada ya kazi hiyo wananchi wa kijiji hicho na vyengine, walisema kuwa walisubiri huduma ya umeme tokea mwaka 1993 mara baada ya kuwekewa laini kubwa ya umeme.
Mohamed Omar Hamad (55) alisema kuwa hata hivyo ameliharakisha shirika la Umeme juu ya kuweka waya mdogo kijijini hapo, ili kila mwananchi mwenye uwezo aweze kuvuta badala ya kuwepo kwa transfoma kama pambo.
‘’Mje tena mtufungie waya mdogo, ili wenye uwezo wavute umeme na sisi tunywe juisi baridi kama mnavykunywa nyinyi huko mijini mtokeako’’,alifafanua na kusema kuwa iwapo watafungiwa waya huyo watavuta majumbani mwao.
Nae kijana Chande Khamis Rashid (28) aliwataka vijana wenzake kuanza kujipanga ili huduma hiyo ya umeme iwawezeshe kujiajiri ikiwa ni pamoja na kuanzisha viwanda vidogo vidogo, saluni pamoja na maduka ya vinywaji baridi.
‘’Vijana wenzangu umeme sasa tayari maana tumeshawekewa trasfoma mpya sasa kilichobakia ni sisi tu ndio wakujipanga ili kuona huduma hii inatunufaisha kwa kuweza kujiajiri ‘’,alifafanua kijana huyo.
Kijiji cha Kichaka na vijiji jirani kwenye Jimbo la Kiwani Wilaya ya Mkoani, vilipitiwa na laini kubwa ya umeme tokea mwaka 1994 uliosambaaza na kampuni na NEREMKO bila ya kuwepo kwa transfoma, hadi mwaka huu walipoamua kuchangana fedha na kufungia mashine hiyo.
Shirika la umeme tawi la Pemba katika mwaka huu, tayari limeshafunga transfoma zaidi ya tano kwa vijiji kadhaa ikiwa ni pamoja na Msuka, Wambaa, Kichaka ambapo zoezi hilo hutokana na wananchi wenyewe kulisaidia gharama shirika la umeme

No comments:

Post a Comment