Social Icons

rss feed facebook twitter google plus linkedin youtube email

Sunday, March 10, 2013

Uhuru Kenyatta achaguliwa kuwa rais wa Kenya


Uhuru Kenyatta achaguliwa kuwa rais wa Kenya  Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka ya Kenya (IEBC) imemtangaza Uhuru Kenyatta kuwa mshindi wa kiti cha rais katika uchaguzi uliofanyika wiki iliyopita.
Kwa mujibu wa matokeo ya uchaguzi wa Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta mgombea wa kiti cha urais kwa tiketi ya Muungano Jubilee ameshinda uchaguzi huo katika mchuano mkali na mpinzani wake Raila Odinga wa mrengo wa Cord. Uhuru Kenyatta amepata asilimia 50.07 na mpinzani wake wa karibu yaani Waziri Mkuu Raila Odinga amepata asilimia 43.28 ya kura zote.
Uhuru ni mwana wa Jomo Kenyatta shujaa wa ukombozi wa Kenya, na sasa anashika hatamu za kuongoza Kenya baada miaka 50 tangu nchi hiyo ipate uhuru.  Uhuru Kenyatta ameweza kumshinda mpinzani wake mkuu Raila Odinga kwa kumpita kwa kura laki nane katika uchaguzi wa rais uliofanyika tarehe 4 mwezi huu. Mchuano mkali uliokuwepo kati ya wagombea hao wawili uliwafanya weledi wa mambo watabiri uwezekano wa uchaguzi huo kuingia katika duru ya pili hapo tarehe 11 mwezi Aprili. 

Matokeo ya chunguzi mbalimbali za maoni pia ambazo zilikuwa zikionyesha tofauti ya kura ya silimia 40 ya Kenyatta na 33 ya Odinga, yalizidisha uwezekano wa kushinda Uhuru Kenyatta katika uchaguzi huo. Muungano wa vyama vilivyomuunga mkono Raila Odinga, CORD umesema utakwenda mahakamani baada ya Uhuru Kenyatta kutangazwa mshindi.
Wakati huo huo serikali ya Kenya imeimarisha ulinzi na usalama na kutayarisha polisi laki moja ili kuzuia uwezekano wa kukaririwa matukio ya umwagaji damu kama yale yaliyotokea katika uchaguzi mkuu uliopita.
Weledi wa mambo wanaamini kuwa uchaguzi mkuu wa sasa wa Kenya ni hatua kubwa mbele katika njia ya demokrasia licha ya dosari za hapa na pale zilizojitokeza katika mfumo mpya wa kupiga kura kwa njia ya elektroniki.
Katika uchaguzi wa mwaka huu Raila Odinga alitaka kutekelezwa uadilifu ambao anasema haukutekelezwa katika uchaguzi wa mwaka 2007.  Odinga ambaye anatoka katika kabila la Luo na anayetambulika kama mzalendo na mwanaharakati wa siku nyingi, aliendesha kampeni za uchaguzi kwa shaari za "Amani". Hata hivyo inaonekana kuwa mpinzani wake, Uhuru Kenyatta amefanikiwa zaidi kuwavutia wapiga kura kwa kutumia nara za "Marekebisho na Mustakbali Mwema kwa Ajili ya Kizazi cha Vijana". Huenda wapigaji kura vijana waliona kuwa matarajio yao yanaweza kutimia kupitia ushindi wa Uhuru Kenyatta mwenye umri wa 51 na si Raila Odinga mwenye umri wa miaka 68.
Alaa kullihal, Uhuru Kenyatta na mgombea mwenza wake William Ruto wanapaswa kujitayarishwa kwa ajili ya kujibu mashtaka ya kuhusika na jinai zilizotokea baada ya uchaguzi mkuu wa mwaka 2007 katika Mahakama ya Kimataifa ya Jinai (ICC) huko Hague nchini Uholanzi. Uhuru anawajibika kufika mahakamani tarehe 9 Julai mwaka huu na makamu wake mtarajiwa William Ruto atafika mahakamani tarehe 28 mwezi huo huo. Uhuru amesema kuwa atashirikiana na mahakama ya ICC hata kama kesi yake itachukua muda mrefu na kulazimika kuwa nje ya nchi kwa kipindi kirefu. Suala hilo ndilo lililotumiwa na wafuasi wa Raila Odinga katika kampeni za uchaguzi wakiwa na matarajio kwamba lingeweza kuwashawishi Wakenya kumpigia kura kiongozi wao.  

No comments:

Post a Comment