Social Icons

rss feed facebook twitter google plus linkedin youtube email

Thursday, September 13, 2012

Maandamano dhidi ya Marekani huko Misri



Misri kwa mara nyingine tena imeshuhudia maandamano ya wananchi dhidi ya Marekani. Maelfu ya Wamisri wameandamana mbele ya ubalozi wa Marekani huko Cairo mji mkuu wa Misri na kuichoma moto bendera ya Marekani. Wafanya maandamano wametaka pia kufungwa ubalozi wa Marekani  huko Misri na kuondoka balozi wa Marekani nchini humo. Wananchi wa Misri wamefanya maandamano hayo wakilalamikia kutengenezwa filamu ya Kimarekani inayomvunjia heshima Mtume Muhammad (s.a.w). Sambamba na Misri, huko Libya pia baadhi ya waaandamanaji wameuvamia ubalozi mdogo wa Marekani huko katika mji wa Benghazi ambapo imeelezwa kuwa, mfanyakazi mmoja wa ubalozi huo raia wa Marekani ameuawa na mwingine kujeruhiwa. Japokuwa  hii si mara ya kwanza kwa Wamarekani kuzivunjia heshima itikadi za Waislamu, lakini kwa kuzingatia hali maalumu ya sasa katika eneo la Mashariki ya Kati, baadhi ya duru za kisiasa zinaamini kuwa, kuchaguliwa kipindi hiki kwa ajili ya kutengeneza filamu hiyo inayomvunjia heshima Mtume wa Uislamu ni jambo lililoratibiwa na halikutokea sadfa. Kwa ibara nyingine ni kuwa watengenezaji wa filamu hiyo inayomvunjia heshima Mtume Muhammad (s.a.w) wamefanya hivyo ili kuzusha hitilafu na mivutano kati ya nchi za Kiarabu zilizoshuhudia mapinduzi ya wananchi hivi karibuni. Wataalamu wengi wa masuala ya kisiasa wanaamini kuwa  kwa kuzingatia kwamba idadi kadhaa ya watu wa kabila la Kibti la Misri wenye misimamo mikali wameshirikiana na Tery Jones Kasisi wa Kimarekani mwenye chuki dhidi ya dini ya Kiislamu kutengeneza filamu inayomvunjia heshima Mtume wa Uislamu, lengo la hatua hiyo ni kuzusha vita baina ya Waislamu na kabila la Kibti la Misri.  Hasa ikizingatiwa kuwa baadhi ya Wakibti wa Misri hawajafurahishwa na kile kinachojiri sasa katika uga wa kisiasa wa nchi hiyo yaani kuingia madarakani wanaharakati wa Kiislamu nchini humo. Itakumbukwa kuwa Kasisi Tery Jones huko nyuma alikabiliwa na wimbi kubwa la malalamiko ya Waislamu kutokana na kitendo chake cha kishenzi cha kuchoma moto nakala kadhaa za kitabu Kitukufu cha Qur'ani. Hakuna shaka kuwa, hivi sasa pia baadhi ya pande zinafanya kila linalowezekana ili kuitumbukiza Misri katika hali ya mchafukoge na hivyo kunufaika na hali hiyo ya kutokuweko uthabiti nchini humo. Marekani na utawala wa Kizayuni zinafahamu vyema kwamba Misri mpya inatofautiana sana na ile ya zama za dikteta Husni Mubarak, zama ambazo Misri ilikuwa ikifuata kibubusa siasa za Tel Aviv na Washington. Hii ni kwa sababu tofauti hizo zimeathiri pakubwa maslahi ya Marekani na utawala wa Kizayuni huko Misri.

No comments:

Post a Comment