Social Icons

rss feed facebook twitter google plus linkedin youtube email

Tuesday, January 22, 2013

Sitta: Katiba ijayo ya Tanzania iwabane mafisadi


Samuel John Sitta, Waziri wa Afrika Mashariki wa Tanzania.
Samuel John Sitta, Waziri wa Afrika Mashariki wa Tanzania.Waziri wa Afrika Mashariki wa Tanzania Samuel Sitta amependekeza kuwa, Katiba mpya ya Tanzania itaje moja ya sifa za wagombea Urais kuwa ni uadilifu ili kuwabana watu ambao wamejilimbikizia mali na wezi kuongoza nchi.  Samuel Sitta amependekeza pia kuwa, Katiba mpya ijayo iweke idadi ya wabunge badala ya kugawa majimbo kila baada ya uchaguzi, jambo ambalo alisema ni kuwaongezea ulaji baadhi ya watu. Mwanasiasa huyo ambaye amewahi kuwa Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania amesisitiza kuwa,
Katiba ijayo ya Tanzania inapaswa kutambua haki za kijamii na haki  za wengi kuliko ilivyo sasa ambapo Katiba inatambua haki ya mtu mmoja mmoja. Hayo yanajiri katika hali ambayo, mchakato wa ukusanyaji maoni kwa ajili ya Katiba mpya ya Tanzania unaendelea nchini humo. Hivi karibuni Mwenyekiti wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba nchini Tanzania alijikuta mashakani baada ya kutoa agizo la kupinga kutolewa baadhi ya maoni na wananchi. Jaji Mstaafu Joseph Warioba anayeongoza tume hiyo yenye dhima ya kukusanya maoni kuhusu katiba mpya aliagiza maafisa kutopokea maoni ya makundi maalumu. Warioba alisema watu watoe maoni yao binafsi bila kufungamana na makundi yoyote. Hatua hiyo imemuweka pabaya jaji huyo mstaafu baada ya makundi ya kutetea haki za binadamu kusema kuwa, agizo hilo ni ukiukaji wa haki ya kujieleza.

No comments:

Post a Comment