Social Icons

rss feed facebook twitter google plus linkedin youtube email

Wednesday, October 2, 2013

Ash Shabab watishia tena kushambulia Kenya


Ash Shabab watishia tena kushambulia Kenya
Kundi la wanamgambo wa ash Shabab la Somalia limetishia kufanya mashambulizi mengine makali nchini Kenya ikiwa ni siku chache tu baada ya kundi hilo kuua makumi ya watu katika jumba la biashara la Westgate, mjini Nairobi. Wanamgambo hao wamedai kama tunavyonukuu taarifa yao kwamba: "Tutawashambulia Wakenya katika sehemu ambazo zitawaumiza zaidi, na tutaigeuza miji yao kuwa makaburi, na mito ya damu itatiririka mjini Nairobi." Vitisho hivyo vya ash Shabab vimekuja baada ya Kenya kukataa kuondoa wanajeshi wake nchini Somalia. Katika taarifa yake hiyo, wanamgambo wa ash Shabab aidha wamesema kama ninavyowanukuu: "Uamuzi wa serikali ya Kenya wa kuendelea kuweka vikosi vyake nchini Somalia ni dalili kuwa hawakupata somo linalotakiwa katika mashambulizi ya Westgate." Hivi karibuni, karibu watu 70 waliuliwa na wanamgambo wa ash Shabab wakati wanamgambo hao walipovamia jumba la biashara la Westgate mjini Nairobi na hadi hivi sasa hatima ya makumi ya watu wengine haijajulikana. Hivi sasa kuna wanajeshi 4,000 wa Kenya kusini mwa Somalia ambako wanapambana na wanamgambo wa ash Shabab wenye mfungamano na mtandao wa al Qaida. Wanajeshi wa Kenya wako nchini Somalia kama sehemu ya kikosi cha Umoja wa Afrika kinacholinda amani nchini humo.