Social Icons

rss feed facebook twitter google plus linkedin youtube email

Saturday, October 12, 2013

'Watanzania ni miongoni mwa watu wasio na furaha'


'Watanzania ni miongoni mwa watu wasio na furaha'
Ripoti iliyotolewa na Umoja wa Mataifa inaonesha kuwa, Watanzania ni miongoni mwa watu wasio na furaha na waliokata tamaa hapa duniani. Ripoti hiyo imeitaja Tanzania kuwa ni miongoni mwa nchi 10 za mwisho duniani kati ya nchi 156 zilizofanyiwa utafiti huo. Upatikanaji wa huduma za jamii, mtazamo wa watu kuhusu rushwa, umri wa kuishi, ukosefu wa kazi, pato la taifa na ukarimu wa watu katika nchi husika, ni baadhi ya vigezo vilivyoangaliwa wakati wa kuandaa ripoti hiyo. Taarifa hiyo imezitaja nchi tano za Denmark, Norway, Uswisi, Uholanzi na Sweden kuwa ndizo zinazoongoza kwa watu wake kuwa na furaha zaidi duniani, huku Angola ikishika nafasi ya kwanza Afrika na ya 61 duniani. Kwa upande wa Afrika Mashariki, wananchi wa Uganda ndio walionekana kuwa na furaha zaidi katika ripoti hiyo kwani nchi hiyo imeshika nafasi ya 120 wakifuatiwa na Kenya iliyoshika nafasi ya 123, Tanzania nafasi ya 151, Rwanda nafasi ya 152 na Burundi ni ya mwisho Afrika Mashariki huku ikiwa inashikilia nafasi ya 153 duniani. Hata hivyo, Waziri wa Kazi na Ajira wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Gaudensia Kabaka ameeleza kushtushwa na ripoti hiyo akisema kuwa ni asilimia 11.7 tu ya Watanzania wasio na ajira na kwamba, wale wanaofanya kazi, wanapata huduma zote za msingi, ikiwa ni pamoja na kwenda likizo na mishahara inayolingana na taaluma zao na kusisitiza kwamba, hafahamu ni vigezo vipi vimetumika katika ripoti hiyo.