Social Icons

rss feed facebook twitter google plus linkedin youtube email

Saturday, October 12, 2013

Njama ya kujenga hekalu Quds tukufu yalaaniwa


Njama ya kujenga hekalu Quds tukufu yalaaniwaTaasisi mbalimbali za Palestina zimelaani njama ya utawala wa Kizayuni wa Israel ya kutaka kujenga hekalu katika eneo la mashariki ya msikiti mtukufu wa al Aqsa. Baraza Kuu la Kiislamu, Baraza la Waqfu na Masuala ya Kiislamu na Baraza la Fatwa la Quds tukufu yametoa taarifa ya pamoja leo ambapo mbali na kufichua, yamelaani pia njama hiyo ya utawala wa Kizayuni dhidi ya kibla cha kwanza cha Waislamu. Taarifa hiyo imeashiria kubadilishwa sura ya sehemu ya msikiti huo ya al Buraq na vilevile kujengwa njia ya mabasi yaendayo kwa kasi katika eneo la kati ya Jabalu-turi na Babul-asbat, na kueleza kuwa miradi hiyo inatekelezwa kwa lengo la kuyayahudisha maeneo matakatifu na kufuta athari za Kiislamu, kitu ambacho hakikubaliki. Taarifa ya taasisi hizo za Palestina imeashiria mpango wa Israel wa kujenga hekalu katika eneo la sehemu moja ya tano ya msikiti wa Alqsa na kusisitiza kwamba msikiti huo kidini, kisiasa na kimamlaka hauna uhusiano wowote na Mayahudi na kwamba eneo hilo takatifu la Baitul Muqaddas ni milki ya Waislamu wote duniani. Sambamba na kutoa indhari kwa utawala wa Kizayuni juu ya mas-ulia utakayobeba kwa hatua yoyote ya kuuvunjia heshima msikiti mtukufu wa al Aqsa, taarifa hiyo imetoa wito pia kwa Ulimwengu wa Kiislamu na wa Kiarabu kutimiza wajibu walionao juu ya msikiti huo mtakatifu pamoja na Quds tukufu…/