Social Icons

rss feed facebook twitter google plus linkedin youtube email

Monday, October 15, 2012

Al Shabaab warudi nyuma huko kusini mwa Somalia


Al Shabaab warudi nyuma huko kusini mwa Somalia
Jeshi la serikali ya Somalia na askari wa kulinda amani wa Umoja wa Afrika (AU) walioko nchini humo wamefanikiwa kukomboa mji mwingine wa kusini mwa Somalia kutoka chini ya udhibiti wa kundi la waasi wa al Shabaab.
Askari wa serikali ya Somalia wanaosaidiwa na jeshi la Kenya chini ya mwavuli wa kikosi cha Umoja wa Afrika (AMISOM) wanaendeleza operesheni ya kukomboa maeneo yaliyokuwa chini ya udhibiti wa jeshi la al Shabaab. Operesheni hiyo ya AMISOM ilipelekea kukombolewa mji wa kistratejia wa Kismayu tarehe 29 Septemba.
Kuondoa wapiganaji wa al Shabaab katika mji huo kumetajwa na wachambuzi wengi wa mambo kuwa ni mafanikio makubwa zaidi ya serikali ya Somalia na Umoja wa Afrika.

Bandari ya Kismayu ilikuwa ikitumiwa kama kitegauchumi kikuu cha al Shabaab ambacho pato lake lilikuwa likitumiwa na kundi hilo kwa ajili ya kununulia silaha na zana za kivita. Kwa msingi huo wachambuzi wa mambo wanasema kukombolewa mji wa Kismayu ni pigo kubwa kwa kundi la al Shabaab. Kukombolewa mji huo pia kumekuwa sababu ya kufungwa shughuli za redio ya kundi hilo iliyokuwa ikirusha matangazo yake kutoka Kismayu.
Baada ya Kismayu, askari wa Somalia na Umoja wa Afrika wamefanikiwa kukomboa mji wa Wanla Weyn ulioko karibu na Mogadishu. Waziri wa Ulinzi wa Somalia ametangaza kuwa, kukombolewa mji huo kumerahisisha tena mawasiliano kati ya miji ya Mogadishu na Baidoa. Hussein Issa amesema kukombolewa Wanla Weyn ni ushindi muhimu kwa serikali ya Somalia ambao utazuia wapiganaji wa al Shabaab na kuimarisha amani katika maeneo mengine ya nchi hiyo.
Jeshi la Umoja wa Afrika linashirikiana na vikosi vya jeshi la serikali ya Somalia kwa shabaha ya kuisaidia serikali ya nchi hiyo kukomboa maeneo yote yanayodhibitiwa na kundi la waasi wa al Shabaab. Serikali mpya ya Somalia inayoongozwa na Rais Hussein Sheikh Muhamuod imeahidi kurejesha amani na kudumu katika maeneo yote ya nchi hiyo.

No comments:

Post a Comment