Social Icons

rss feed facebook twitter google plus linkedin youtube email

Thursday, October 25, 2012

Viongozi wa Uamsho waongezewa mashtaka, wakosa dhamana warudishwa rumande



Kiongozi wa Jumuiya ya UAMSHO Sheikh Farid Hadi Ahmed kushoto akiwa na wenzake sita walioletwa Mahakama kuu Zanzibar Vuga wakiwa hawana ndevu na kufunguliwa mashtaka manne mapya mahakamani hapo yakiwemo kuharibu mali za watu zenye thamani ya Shl.Milioni 50 na kufanya vurugu za makusudi zakuhatarisha amani katika nchi


Baadhi ya Askari wa kutuliza fujo wakiwa Mahakama kuu Zanzibar Vuga kwa lengo la kutuliza amani Mahakamani hapo



Baadhi ya Viongozi wa Jumuiya ya UAMSHO wakiwa wanatoka katika Mahakama Kuu ya Zanzibar Vuga baada ya kufunguliwa mashtaka manne mapya..

Mawakili wa Viongozi wa Jumuiya ya UAMSHO Abdallah Juma kushoto na Salim Tawfik wakizungumza na waandishi wa habari kuhusu kujitoa kwao siku ya leo katika kesi hiyo kutokana na usmbufu wanaofanyiwa wateja wao wa kuhawangaishwa na kukosa kupelekwa Mahakama ya Kwerekwe kwa muda muafa.Picha na Makame Mshenga-Maelezo Zanzibar

VIONGOZI wakuu wa jumuia ya uamsho na mihadhara ya kiislamu Zanzíbar (JUMIKI), wamenyimwa dhamana katika mashtaka mapya waliyosomewa leo katika mahakama ya mkoa Vuga mjini Zanzíbar.
Hayo yamefahamika mbele ya mrajis wa mahakama kuu Zanzíbar George Joseph Kazi, wakati viongozi hao wakiwa na wafuasi wao watano walipofikishwa mahakamani hapo kwa ajili ya kusomewa mashtaka yanayowakabili.
Washtakiwa hao walifikishwa mbele ya mrajis wa mahakama kwa ajili ya kusomewa mashtaka mapya yaliyowasilishwa na mkurugenzi wa mashtaka Zanzíbar (DPP) yanayohusiana na matukio mbalimbali ya uharibifu wa mali, uchochezi, kumficha Sheikh Farid pamoja na la kumtukana Kamishna wa Polisi wa Zanzíbar.
 


Katika mashtaka hayo ambayo waliyakana, upande wa mashtaka ulipinga ombi la washtakiwa hao kupatiwa dhamana.
Mbali na Farid Hadi Ahmed, washtakiwa wengine ni Mselem Ali Mselem, Mussa Juma Issa, Azan Khalid Hamdan, Suleiman Juma Suleiman, Khamis Ali Suleiman, Hassan Bakari Suleiman na Ghalib Ahmada Omar.
Wote hao wameshtakiwa kwa makosa ya uvunjaji wa amani, ushawishi wa kuchochea na kurubuni watu, kula njama pamoja na shitaka la kufanya kitendo kinachoweza kuleta uvunjifu wa amani lililokuwa likimkabili Azan Khalid Hamdan pekee.
Washtakiwa hao waliomba mahakama hiyo, iwapatie dhamana kwa madai kuwa ni haki yao ya kimsingi kwa mujibu wa sheria na katiba kwani mashtaka yanayowakabili si miongoni mwa makosa yasiyokuwa na dhamana.
Wakipinga ombi hilo, jopo la wanasheria wa serikali kutoka Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka wakiongozwa na Raya Issa Mselem, waliiomba mahakama hiyo isiwapatie dhamana.
Akiwasilisha hati ya pingamizi hiyo iliyosainiwa na DPP Ibrahim Mzee Ibrahim, kwa mujibu wa kifungu cha 19 (1) (2) cha sheria za usalama wa taifa sura ya 47, sheria ya mwaka 2002, Raya alifahamisha kuwa, kwa mujibu wa uwezo aliopewa DPP chini ya kifungu hicho anawafungia dhamana washtakiwa hao.
Alisema kuwa, sheria hiyo imempa uwezo DPP kumfungia dhamana mshtakiwa yeyote ikiwa ataona ipo haja hiyo kwa maslahi ya umma.
Akitoa uamuzi wake baada ya kusikiliza hoja za pande Mbili hizo, mrajis George Joseph Kazi, alisema kuwa, amelazimika kuwanyima dhamana washtakiwa hao kutokana na hati iliyowaslishwa na DPP chini ya kifungu cha 19 (1) na (2) cha sheria za usalama wa taifa sura ya 47 ya mwaka 2002.
Katika hatua nyengine, mawakili wawili wa washtakiwa hao, Abadalla Juma na Salum Taufik, walifika katika mahakama hiyo lakini baada ya wateja wao kushindwa kuwasilishwa kwa wakati hadi saa tano za asubuhi, mawakili hao walitangaza kujitoa katika kesi hiyo.
Walidai hatua yao hiyo imetokana na kutokuwepo mashirikiano kati ya pande mbili hizo, hali inayoonesha kuwepo njama za makusudi zinazofanywa dhidi ya wateja wao.
Kesi hiyo imeakhirishwa hadi tarehe 7 Novemba mwaka huu.
NA IDARA YA HABARI MAELEZO ZANZIBAR

No comments:

Post a Comment