Social Icons

rss feed facebook twitter google plus linkedin youtube email

Monday, October 15, 2012

Siku Kumi Bora Kabisa Za Allaah

Inatupasa tumshukuru Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) kwa neema Aliyotujaalia ya kutuwekea miezi mitukufu, au siku tukufu au nyakati tukufu ambazo vitendo vyake vyema huwa na thawabu nyingi sana. Na hivi tunakaribia kabisa kuingia katika mwezi mwingine mtukufu wa Dhul-Hijjah. Katika mwezi huu, siku kumi za mwanzo ni siku bora kabisa katika dunia na zina fadhila kubwa kutokana na dalili zifuatazo:
                                            

عن ابن عباس رضي الله عنهما، أن النبي صلى الله عليه وسلم قال: ((ما من أيام العمل الصالح فيها أحب إلى الله من هذه الأيام)) - يعني أيام العشر-. قالوا: يا رسول الله، ولا الجهاد في سبيل الله ؟ قال: ((ولا الجهاد في سبيل الله، إلا رجل خرج بنفسه وماله ثم لم يرجع من ذلك بشيء)) البخاري

Imetoka kwa Ibn Abbaas (Radhiya Allaahu 'anhuma) kwamba Mjumbe wa Allaah amesema: ((Hakuna siku ambazo vitendo vyake vyema Anavipenda Allaah kama siku kumi hizi)) (siku kumi za mwanzo wa mwezi wa Dhul-Hijjah) Akaulizwa, je, hata Jihaad katika njia ya Allaah? Akajibu (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) ((Hata Jihaad katika njia ya Allaah isipokuwa mtu aliyekwenda na nafsi yake na mali yake ikawa hakurudi na kimojawapo)) [Al-Bukhaariy]

Zifuatazo ni fadhila kuu za masiku hayo kumi ya Dhul-Hijjah. Na lau ee ndugu Muislamu utakapojipwekesha katika ibaada na kutenda amali njema zenye ikhlaas na zinazotokana na mafunzo Sahihi ya Sunnah za Mtume (Swalla-Allaahu ‘alayhi wa aalihi wa sallam), basi bila shaka utajichumia thawabu maradufu na ambazo zitakuwa nzito
In Shaa Allaah katika mizani yako.


Allaah Ameziapia Siku Kumi Hizi



Kwa jinsi zilivyokuwa na umuhimu mkubwa siku hizo kumi, hadi kwamba Allaah (Subhaanah wa Ta'ala) Ameziapia katika Qur-aan Anaposema:



بِسْمِ اللّهِ الرَّحْمَنِ الرَّحِيمِ ((وَالْفَجْرِ)) ((وَلَيَالٍ عَشْرٍ))

BisimiLLaahir-Rahmaanir-Rahiym. ((Naapa kwa Alfajiri)) ((Na kwa masiku kumi)) [Al-Fajr: 1-2].


Wanavyuoni wafasiri wa Qur-aan wamekubaliana kwamba zilokusudiwa hapo ni Siku kumi za Dhul-Hijjah.





Siku Za Manufaa Na Kumkumbuka Allaah


Inapasa kumdhukuru mno Allaah (Subhaanah wa Ta’ala) kwa kukumbuka Neema Zake zisizohesabika:


((لِيَشْهَدُوا مَنَافِعَ لَهُمْ وَيَذْكُرُوا اسْمَ اللَّهِ فِي أَيَّامٍ مَّعْلُومَاتٍ))


((Ili washuhudie manufaa yao na kulitaja Jina la Allaah katika siku zinazojulikana)) [Al-Hajj: 28].


 Ibn ‘Abbaas kasema: “Hizo ni siku kumi za Dhul-Hijjah” . Na Amesema: “Manufaa ya dunia hii na ya Akhera” . Manufaa ya Akhera yanajumuisha kupata Radhi za Allaah. Manufaa ya vitu vya dunia inajumuisha wanyama wa kuchinjwa na biashara. [Tafsiyr Ibn Kathiyr].



  
Amali Zake Ni Bora Kuliko Kwenda Katika Jihaad Fiy SabiliLLaah



Kutokana na ilivyotajwa katika usimulizi wa Hadiyth ifuatayo, kwamba amali yoyote utendayo katika masiku kumi hayo, ni bora kuliko kwenda kupigana jihadi vitani. Ukizingatia kwenda kupigana jihadi ni jambo zito mtu kuliitikia, kwani huko kuna mashaka mbali mbali, ikiwemo khofu ya kujeruhiwa na kupoteza viungo vya mwili, kufariki, kupoteza mali n.k. Ila hilo si zito kwa mwenye imani ya hali ya juu kabisa kutaka kuyakabili mashaka hayo na kutamani kufa shahidi. Kwa hiyo usidharau amali yoyote hata iwe ndogo vipi itekeleze kwani Allaah Subhaana wa Ta'ala ni Al-Jawwaad (Mwingi Wa Ukarimu), Al-Kariym (Karimu), Al-Wahhaab (Mwingi Wa Kutunuka, Mpaji Wa Yote), Al-Majiyd (Mwingi Mno Wa Vipawa Na Ukarimu).



عن ابن عباس رضي الله عنهما، أن النبي صلى الله عليه وسلم قال:)) ما من أيام العمل الصالح فيها أحب إلى الله من هذه الأيام)) - يعني أيام العشر-. قالوا: يا رسول الله، ولا الجهاد في سبيل الله ؟ قال: ((ولا الجهاد في سبيل الله، إلا رجل خرج بنفسه وماله ثم لم يرجع من ذلك بشيء)) البخاري


Imetoka kwa Ibn 'Abbaas (Radhiya Allaahu 'anhuma) kwamba Mjumbe wa Allaah amesema: ((Hakuna siku ambazo vitendo vyake vyema Anavipenda Allaah kama siku kumi hizi)) (siku kumi za mwanzo wa mwezi wa Dhul-Hijjah) Akaulizwa, je, hata Jihaad katika njia ya Allaah? Akajibu (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) ((Hata Jihaad katika njia ya Allaah isipokuwa mtu aliyekwenda na nafsi yake na mali yake ikawa hakurudi na kimojawapo)) [Al-Bukhaariy].


   

Ibada Zote Zimejumuika Katika Siku Hizi



Ibada zote zimejumuika katika siku kumi hizi nazo ni Swalah, Swawm, Swadaqah, Hajj, wala hazijumuiki hizi wakati mwingine.



Vitendo Vyema Vya Kutenda Katika Siku Kumi Hizi



1- Kutekeleza Hajj na 'Umrah (kwa mwenye uwezo)

  
عن أبي هريرة رضي الله عنه أن رسول الله صلى الله عليه وسلم قال ((العمرة إلى العمرة كفارة لما بينهما . والحج المبرور ليس له جزاء إلا الجنة)) أخرجه البخاري و مسلم


Imetoka kwa Abu Hurayrah (Radhiya Allaahu 'anhu) kwamba Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) kasema: (('Umrah hadi 'Umrah hufuta (madhambi) baina yake, na Hajjum-Mabruur haina jazaa ila Pepo)) [Al-Bukhaariy na Muslim].



عن أبي هريرة رضي الله عنه قال: "سئل رسول الله صلى الله عليه وسلم: أي الأعمال أفضل؟ قال: ((إيمان بالله ورسـوله)). قيل: ثم مـاذا؟ قال: ((الجهاد في سبيل الله)) قيل: ثم ماذا؟ قال: ((حج مبـرور)) متفق علية

Imetoka kwa Abu Hurayrah(Radhiya Allaahu 'anhu) ambaye amesema: "Aliulizwa Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amali gani ni bora kabisa?" Kasema: ((Kumuamini Allaah na Mtume Wake)), Akaulizwa:"Kisha nini?" Kasema: ((Jihaad katika njia ya Allaah)). Akaulizwa: "Kisha nini?" Kasema: ((Hajj Mabruur)) [Al-Bukhaariy na Muslim].



2- Kuomba Tawbah ya kweli na kujiepusha na maasi


Anasema Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala):


(( يَا أَيُّهَا الَّذِينَ آمَنُوا تُوبُوا إِلَى اللَّهِ تَوْبَةً نَّصُوحًا))

((Enyi mlioamini! Tubuni kwa Allaah toba iliyo ya kweli!)) [At-Tahriym: 8].

Na Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) ametupa matumaini makubwa ya kufutiwa madhambi na makosa yetu katika usimulizi ufuatao:
     
عن أنس رضي الله عنه قال: سمعت رسول الله صلى الله عليه وسلم يقول: ((قال الله: يا ابن آدم إنك ما دعوتني ورجوتني غفرت لك على ما كان منك ولا أبالي، يا ابن آدم لو بلغت ذنوبك عنان السماء، ثم استغفرتني غفرت لك ولا أبالي، يا ابن آدم إنك لو أتيتني بقراب الأرض خطايا، ثم لقيتني لا تشرك بي شيئاً لأتيتك بقرابها مغفرة)) أخرجه الترمذي وحسنه الألباني في الصحيحة

Kutoka kwa Anas (Radhiya Allaahu 'anhu): "Nimemsikia Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) akisema: ((Allaah Amesema: Ee Mwana Adam! Hakika ukiniomba na ukanitaraji (kwa malipo) Nitakusamehe yale yote uliyonayo na wala Sijali, Ee Mwana Adam! Lau zingefikia dhambi zako ukubwa wa mbingu, kisha ukaniomba maghfira, Ningekughufuria bila ya kujali (kiasi cha madhambi uliyoyafanya). Ee Mwana Adam, Hakika ungenijia na madhambi yakaribiayo ukubwa wa ardhi, kisha ukakutana nami na hali hukunishirikisha chochote, basi Nami Nitakujia na msamaha unaolingana nao)) [Imetolewa na At-Tirmidhiy na Shaykh Al-Albaaniy kaipa daraja ya Hasan].



3- Kumkumbuka sana Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala)


Kwa Tasbiyh, Tahmiyd, Tahliyl, Takbiyr (kusema: Subhaana Allaah, AlhamduliLlaah, Laa Ilaaha Illa Allaah, Allaahu Akbar)


عن ابْنِ عُمَرَ عَنِ النَّبِيِّ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ قَال: (( مَا مِنْ أَيَّامٍ أَعْظَمُ عِنْدَ اللَّهِ وَلَا أَحَبُّ إِلَيْهِ مِنَ الْعَمَلِ فِيهِنَّ مِنْ هَذِهِ الْأَيَّامِ الْعَشْرِ فَأَكْثِرُوا فِيهِنَّ مِنَ التَّهْلِيلِ وَالتَّكْبِيرِ وَ التَّحْمِيدِ )) أخرجه أحمد

Imetoka kwa ibn 'Umar kwamba Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Hakuna siku zilizokuwa tukufu kwa Allaah na zilizokuwa vitendo vyake vipenzi kabisa Kwake kama siku hizi, basi zidisheni Tahliyl na Takbiyr na Tahmiyd)) [Ahmad].


Inavyopasa kufanya takbiyr:


الله أكبر. الله أكبر. لا إله إلا الله. والله أكبر. الله أكبر ولله الحمد

“Allaahu Akbar, Allaahu Akbar, Laa Ilaaha Illa Allaah Wa-Allaahu Akbar, Allaahu Akbar WaliLlaahil-Hamd”


Takbiyr hii ni aina mbili:


Takbiyr Za Nyakati Zote


Takbiyr wakati wote usiku au mchana tokea unapoingia mwezi wa Dhul-Hijjah na inaendelea mpaka siku ya mwisho ya Tashriyq (tarehe 13 Dhul-Hijjah) baada ya magharibi.


Takbiyr Za Nyakati Maalumu


Takbiyr baada ya kila Swalah na huanza asubuhi ya siku ya 'Arafah mpaka baada ya magharibi ya siku ya mwisho ya Tashriyq.


4- Kufufua Sunnah ya Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)


Wanaume wanatakiwa waseme kwa sauti ili kuwakumbusha wengine na kufufua Sunnah ya Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) na wanawake waseme kimya kimya isipokuwa wakiwa na mahaarim wao. Kufufua Sunnah ya Mtume ni muhimu kwani bila ya kufanya hivyo tutakuwa kwanza tunakosa fadhila zake, pili zitapotea Sunnah za kipenzi chetu Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam)


Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) kasema: ((Atakayemuongoza mwenzake kufanya jambo jema atapata thawabu sawa sawa na za yule atakayetenda hilo jambo jema)) [Muslim]


كان ابن عمر وأبو هريرة رضي الله عنهما يخرجان إلى السوق في أيام العشر يكبران، ويكبر الناس بتكبيرهما (البخاري)

Ibn 'Umar na Abu Hurayrah walikuwa wakienda sokoni katika siku kumi na kufanya Takbiyr kwa sauti na watu wakiwaigiza)) [Al-Bukhaariy].


5- Kufunga siku hizi khaswa siku ya 'Arafah



عن أبي سعيد الخضري رضي الله عنه قال: قال عليه الصلاة والسلام ((من صام يوما في سبيل الله باعد الله وجهه عن النار سبعين خريفا) رواه البخاري ومسلم

Kutoka kwa Abu Sa'iydil-Khudhwriyy (Radhiya Allaahu 'anhu) ambaye amesema: Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) kasema: ((Mwenye kufunga siku kwa ajili ya Allaah, basi Allaah Atamuokoa uso wake kutokana na moto kwa umbali wa miaka sabini)) [Al-Bukhaariy na Muslim].


قال صلى الله عليه وسلم : (( كل عمل ابن آدم له الحسنة بعشر أمثالها إلى سبعمائة ضعف . يقول الله عز وجل : إلا الصيام فإنه لي وأنا أجزي به)) أخرجه البخاري ومسلم

Amesema Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) ((Kila amali njema ya mwanaadamu inalipwa mara kumi na inaongezewa thawabu kutoka kumi hadi mia saba, na Allaah Anasema isipokuwa Swawm, kwani hiyo ni kwa ajili Yangu na Mimi Ndiye nitakayemlipa)) [Al-Bukhaariy na Muslim].


6- Kuzidisha vitendo vyema mbali mbali


Mbali ya kutekeleza fardhi ya Swalah kwa kuswali kwa wakati wake, kuswali Sunnah zaidi, kusoma Qur-aan, Swadaqah, Du'aa, kutii wazazi na kuwafanyia wema, kuwasiliana na jamaa (kuunga undugu), kuwafanyia wema jirani, kuamrishana mema na kukatazana maovu, kufanyiana wema na ihsani na kadhalika.


7- Kuchinja baada ya Swalah ya 'Iyd


Anasema Allaah (Subhaanahu Wa Ta'ala):
((فَصَلِّ لِرَبِّكَ وَانْحَرْ))

((Basi Swali kwa ajili ya Mola wako na uchinje)) [Al-Kawthar: 2]


Pia, usimulizi ufuatao tunapata maelezo ya aina ya mnyama wa kuchinja na uchinjaji wake.  


فعَنْ أَنَسٍ رضي الله عنه قَالَ: (( ضَحَّى النَّبِيُّ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ بِكَبْشَيْنِ أَمْلَحَيْنِ أَقْرَنَيْنِ ذَبَحَهُمَا بِيَدِهِ وَسَمَّى وَكَبَّرَ وَوَضَعَ رِجْلَهُ عَلَى صِفَاحِهِمَا )) متفق عليه

Imetokea kwa Anas (Radhiya Allaahu 'anhu) ambaye amesema: "Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alichinja kondoo wawili weupe* wenye pembe, amewachinja kwa mikono yake, akasema BismiLlaah na Allaahu Akbar na akaweka mguu wake upande wa nyuma yao". [Al-Bukhaariy na Muslim].


*Baadhi ya wanachuoni wamesema kuwa ni weupe ulio na alama nyeusi, wengine wamesema uliochanganyika na wekundu.


Kitendo hiki cha kuchinja ni ibada tukufu na ni Sunnah iliyosisitizwa hata wanachuoni wameona kuwa ni WAAJIB kwa kila aliyekuwa na uwezo wa kuchinja.


Yanayompasa kufanya mwenye kutaka kuchinja


Baada ya kutia niyyah ya kuchinja, asikate mtu nywele wala kucha mpaka amalize kuchinja kama tulivyoamrishwa katika Hadiyth ifuatayo:


عن أم سلمة رضي الله عنها، أن النبي صلى الله عليه وسلم قال: (( إذا رأيتم هلال ذي الحجة وأراد أحدكـم أن يضحّي فليمسك عــن شعره وأظفاره)) ، وفي راوية (( فلا يأخذ من شعره ولا من أظفـاره حتى يضحّي )) مسلم

Imetoka kwa Ummu Salamah (Radhiya Allaahu 'anha) kwamba Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Ukiandama mwezi wa Dhul-Hijjah na ikiwa yuko anayetaka kuchinja basi azuie (asikate) nywele zake na kucha zake)


Na katika riwaya nyingine ((Asikate nywele wala kucha mpaka akimaliza kuchinja)) [Muslim na wengineo].


Hii ni fadhila na neema kwetu maana tunakuwa katika hali ya ‘Ihraam’ kama waliokuwa kwenye Hijjah. Ikiwa amesahau mtu, mfano akakata kucha basi aendelee tu na niyyah yake mpaka amalize kuchinja.


8-Kuhudhuria Swalah ya 'Iyd


Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amewahimiza mpaka wanawake walio katika hedhi na wazee waende kusikiliza khutbah ya Swalah. Wakati wa Swalah ukifika, wanawake hao wenye hedhi wajitenge kando hadi itakapomalizika Swalah na kisha wajiunge na wenzao kusikiliza khutbah.

  


Siku Ya ‘Arafah Ni Siku Ya Tisa Dhul-Hijjah



a) Madhambi ya miaka miwili hufutiwa atakayefunga



Siku hii tukufu ni siku iliyokamilika dini yetu. Thawabu za kufunga siku hii ni kufutiwa madhambi ya miaka miwili.


عَنْ أَبِي قَتَادَةَ رضي الله عنه أن النَّبِيَّ صَلَّى اللَّهُ عَلَيْهِ وَسَلَّمَ قَالَ : ((صِيَامُ يَوْمِ عَرَفَةَ أَحْتَسِبُ عَلَى اللَّهِ أَنْ يُكَفِّرَ السَّنَةَ الَّتِي قَبْلَهُ وَالسَّنَةَ الَّتِي بَعْدَهُ )) أخرجه مسلم

 Imetoka kwa Abu Qataadah (Radhiya Allaahu 'anhu) ambaye amesema: Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) kasema kuhusu Swawm ya 'Arafah kuwa ((inafuta madhambi ya mwaka uliopita na wa baada yake)) [Muslim].



b) Siku ambayo huachiliwa watu wengi huru na moto


عن عائشة رضي الله عنها أن رسول الله صلى الله عليه وسلم قال: ((ما من يوم أكثر من أن يعتق الله فيه عبداً من النار من يوم عرفة)) رواة مسلم

Imetoka kwa Mama wa Waumini, 'Aaishah (Radhiya Allaahu 'anhaa) kwamba Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) amesema: ((Hakuna siku Allaah Anayowaacha huru waja na moto kama siku ya ‘Arafah)) [Muslim].



c) Du'aa bora kabisa ni Du'aa katika siku ya Arafah


Vile vile inapasa kumtaja sana Allaah siku hii kama alivyosema Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) kuwa:


((خير الدعاء دعاء يوم عرفة، وخير ما قلت أنا والنبيون من قبلي: لا إله إلا الله وحده لا شريك له، له الملك وله الحمد وهو على كل شيء قدير)) روى الترمذي

((Du’aa bora kabisa ni du’aa katika siku ya 'Arafah, na yaliyo bora kabisa niliyosema mimi na Mitume kabla yangu ni:


'Laa Ilaaha Illa Allaah Wah-dahu Laa Shariyka Lahu, Lahul-Mulku Wa-Lahul-hamdu Wa Huwa 'Alaa Kulli Shay-in Qadiyr’)) [At-Tirmidhiy].




Siku Ya Kuchinja Ni Siku Kuu Ya ‘Iyd


Kasema Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam):


((إن أعظم الأيام عند الله يوم النحر، ثم يوم الْقَرّ)) سنن أبي داود

((Siku iliyo tukufu kabisa kwa Allaah ni siku ya kuchinja, kisha siku ya kutulia)) (yaani siku ya kukaa Minaa) [Abu Daawuud].


  

Siku Za Tashriyq


Ni siku ya kumi na moja na kumi na mbili na kumi na tatu ya Dhul-Hijjah yaani baada ya siku ya 'Iyd. Na siku hizi tatu zimeitwa siku za Tashriyq kwa sababu watu walikuwa wakikatakata nyama na kuzianika juani. Siku za kuanika (nyama) juani. Na pi siku hizi hujulikana kwa 'siku za Minaa'.


a) Kumkumbuka sana Allaah


Katika siku hizi inampasa Muislamu azidishe kumkumbuka Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) kama Anavyosema:

((وَاذْكُرُواْ اللّهَ فِي أَيَّامٍ مَّعْدُودَاتٍ))

((Na mtajeni Allaah katika zile siku zinazohisabiwa)) [Al-Baqarah: 203].


Ibn 'Abbaas kasema: Siku zinazohisabiwa ni siku za Tashriyq (11, 12, 13 Dhul-Hijjah) na Siku zinazojulikana ni siku za kumi za mwanzo za Dhul-Hijjah. [Al-Qurtubiy: 3.3]


b) Haifai kufunga katika siku hizi


Haifai kufunga katika siku hizi hata kama mtu alikuwa na mazowea ya kufunga Sunnah za Jumatatu na Alkhamiys au Ayyaamul-Baydh kutokana na makatazo kama haya:


عن أبي هريرة أن رسول الله صلى الله عليه وسلم بعث عبد الله بن حُذافة يطوف في منى: ((لا تصوموا هذه الأيام، فإنها أيام أكل وشرب، وذكر الله، عز وجل))

Imetoka kwa Abu Hurayrah kwamba Mtume (Swalla Allaahu 'alayhi wa aalihi wa sallam) alimtuma 'Abdullaah bin Hudhaafah azunguke Minsa na atangaze "Msifunge siku hizi, kwani hizi ni siku za kula na kunywa na kumkumbuka Allaah Mwenye Nguvu Mtukufu' [At-Twabariy 4: 211]



Tunamuomba Allaah (Subhaanahu wa Ta'ala) Atupe umri na afya na uwezo wa kuweza kufanya mengi ya kumridhisha katika siku hizi tukufu na siku zote nyingine ili tujipatie thawabu nyingi na Atujaaliye tuwe katika wale wanaosikiliza kauli na daima wakafuata zile zilizo njema. Aamiyin

No comments:

Post a Comment