Social Icons

rss feed facebook twitter google plus linkedin youtube email

Sunday, December 2, 2012

Burkina Faso yasisitiza juu ya oparesheni ya kijeshi kaskazini mwa Mali


Burkina Faso yasisitiza juu ya oparesheni ya kijeshi kaskazini mwa Mali
Waziri wa Mambo ya Nje wa Burkina Faso amesema nchi yake iko tayari kushiriki katika oparesheni ya kijeshi huko kaskazini mwa Mali.
Jibril Bassole amesisitiza juu ya kukombolewa eneo la kaskazini mwa Mali na kusema kuwa wanajeshi wa Burkina Faso wako tayari kushiriki kwenye oparesheni hiyo. Burkina Faso, Niger na Mauritania ni nchi jirani na Mali ambazo zimeathirika zaidi na na mgogoro wa kisiasa, kibinadamu na kiusalama huko kaskazini mwa nchi hiyo. Kamisheni ya Wakimbizi ya Umoja wa Mataifa imetoa mamilioni ya dola kwa ajili ya kuwahifadhi wakimbizi tangu mwanzoni mwa mwaka huu baada ya raia wa kaskazini mwa Mali kulikimbia eneo hilo na kuelekea katika nchi jirani. Uhaba wa chakula na ukosefu wa amani katika eneo la Sahel-Sahara la Afrika umekuwa changamoto kuu kwa nchi za eneo hilo. Katika mazingira hayo, Umoja wa Afrika (AU) na jumuiya ya kieneo ya Ecowas zimeafiki suala la kuanzishwa operesheni ya kijeshi ili kulikomboa eneo la kaskazini mwa Mali linalodhibitiwa na makundi yenye silaha. Baraza la Amani na Usalama la Umoja wa Afrika katikati ya mwezi huu liliwasilisha kwa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa ripoti inayoidhinisha oparesheni hiyo.
Katika hali ambayo wakuu wa AU, ECOWAS na jamii ya kimataifa wanasubiri azimio la Baraza la Usalama kuhusiana na kadhia ya kaskazini mwa Mali, Ban Ki Moon Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa pia ameafiki kwa masharti kutumwa wanajeshi nchini humo. Mpango wa kutuma vikosi vya jeshi chini ya uongozi wa nchi za Kiafrika ili kuiunga mkono serikali ya Mali utajulikana kwa kifupi kwa jina la Afisma. Ban Ki Moon ameeleza kuwa mazungumzo ya pande zote na makundi yanayobeba silaha yenye mfungamanao na makabila ya Tuareg huko kaskazini mwa Mali yanapasa kufanyika kwanza na oparesheni ya kijeshi iwe chaguo la mwisho la kutatua mgogoro wa Mali.
Wakati huo huo ripoti mbalimbali zinaeleza kuwa makundi yenye silaha ya kusini mwa Mali yanawachochea vijana kutoka nchi za Ulaya na za Kiafrika. Makundi hayo ambayo mwaka 1999 yalipambana na jeshi la Mali hivi sasa yanajipanga upya ili kuyakomboa maeneo ya kaskazini chini ya nara" Mali ni Nchi yetu". Licha ya kuweko uhaba mkubwa wa idadi ya wanajeshi katika jeshi la Mali, lakini makundi yenye silaha huko kusini mwa nchi hiyo yanajizuia kujiunga na jeshi na yameazimia kukomboa eneo la kaskazini kwa mapambano yao wenyewe.
Huko kaskazini mwa Mali harakati ya Kitaifa ya Ukombozi wa Azawad ambayo kwa miaka kadhaa inaendesha mapigano dhidi ya jeshi la Mali kwa ajili ya kulikomboa eneo la Azawad hivi sasa imetengwa. Ni vyema kuashiria hapa kuwa wapiganaji wa baadhi ya makundi ya kaskazini mwa Mali kama harakati ya Jihad na Uadilifu ni raia kutoka katika nchi za Algeria, Tunisia, Misri, Sudan na Pakistan pia.
Wachambuzi wa mambo wanaamini kuwa biashara haramu ya madawa ya kulevya, silaha na binadamu katika eneo la Sahel-Sahara imeongezeka tangu kuanza mgogoro wa Mali. Mgogoro wa kaskazini mwa Mali na machafuko ya mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo ni miongoni mwa masuala muhimu yaliyojadiliwa katika mazungumzo ya hivi karibuni huko Washington kati ya Bi Nkosazana Dlamini Zuma, Mkuu wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika, Hillary Clinton Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Marekani na Naibu wake John Carson.

No comments:

Post a Comment