Social Icons

rss feed facebook twitter google plus linkedin youtube email

Thursday, December 20, 2012

24 wauawa katika mapigano Sudan Kusini


24 wauawa katika mapigano Sudan Kusini Watu 24 wameuawa katika mapigano kati ya jeshi la Sudan Kusini na wapiganaji wa kundi la wanamgambo linaloongozwa na mtu aliyejitangazia unabii katika jimbo la Jonglei huko mashariki mwa nchi hiyo. Jeshi la Sudan Kusini limetangaza kuwa liliwashambulia waasi hao wanaoongozwa na Dak Kueth ikiwa ni sehemu ya kampeni ya kuwatomokeza wanamgambo wa makundi ya kikabila katika eneo hilo. Luteni Jenerali Kuol Deim Kuol amesema wanamgambo 19 na askari watano waliuawa katika mapigano hayo.
Mfululizo wa mauaji ya ulipizaji kisasi kati ya makabila ya Murle na Lou Nuer yanayochochewa na wizi wa mifugo yamekuwa yakishuhudiwa huko Jonglei huku serikali ya Juba ikiendesha kampeni ya upokonyaji silaha katika maeneo mbali mbali ya nchi hiyo. Kwa mujibu wa Kuol walipata taarifa kuwa Dak Kueth alikuwa anawahamasisha vijana wa Lou Nuer kwenda kuwashambulia watu wa kabila la Murle huko Akobo ndipo wakaamua kufanya shambulio la kuzuia kutokea hujuma hiyo. Hii ni katika hali ambayo makundi ya kutetea haki za binadamu yanalilaumu jeshi la Sudan Kusini kuwa lilifanya jinai mbali mbali ikiwemo ubakaji na utesaji wakati wa kutekeleza kampeni yake ya upokonyaji silaha mapema mwaka huu…/

No comments:

Post a Comment