Social Icons

rss feed facebook twitter google plus linkedin youtube email

Tuesday, December 11, 2012

Viongozi Uamsho Zanzibar watendewa haki - Wakili


Wakili anayewatetea viongozi wa muungano wa taasisi za Kiislamu maarufu kwa jina la Uamsho visiwani Zanzibar amesema kuwa, viongozi hao wameanza kupatiwa huduma muhimu kama mahabusu wengine katika gereza la Kiinua Mguu mjini Unguja.
Bw. Salum Taufiq amenukuliwa akisema hayo na kuongeza kuwa, wateja wake tayari wameruhusiwa kula chakula kutoka nyumbani, kusoma Qur'ani misahafuni, kubadilisha nguo pamoja na kutoka kwenye vyumba vyao na kuchanganyika na mahabusu wengine.
Miongoni mwa mashtaka yanayowakabili viongozi hao ni kusababisha uharibifu wa mali na kuhatarisha usalama wa taifa na wako kizuizini kwa miezi kadhaa sasa.

Viongozi hao ni maarufu kwa kupigania mabadiliko katika muundo wa muungano wa Tanganyika na Zanzibar na walifanya mikutano mingi kuhamasisha wananchi kukataa mfumo wa hivi sasa wa muungano wa nchi hizo mbili wakisema kuwa si wa kiadilifu.
Viongozi hao wa Uamsho pia wamefungua kesi ya kupinga kubaguliwa na kutopewa huduma bora tangu walipofunguliwa mashtaka tarehe 21 Oktoba mwaka huu.
Hata hivyo upande wa mashtaka umepinga madai hayo na kuitaka Mahakama Kuu ya Zanzibar, kutupilia mbali kesi hiyo iliyofunguliwa na viongozi wanane wa Uamsho, ukidai kwamba kesi hiyo imefunguliwa kinyume cha sheria kutokana na hati ya kiapo kukosa tarehe ya kufunguliwa pamoja na jina la mtu aliyekula kiapo kwa niaba ya washitakiwa hao.
Sheikhe Farid Hadi Ahmed, Sheikh Mselem Ali Mselem, Sheikh Mussa Juma Issa, Sheikh Azzan Khalid Hamdan, Sheikh Suleiman Juma Suleiman, Sheikh Khamis Ali Suleiman, Sheikh Hassan Bakari Suleiman na Sheikh Gharib Ahmada Omar ndio waliofungua kesi hiyo.

No comments:

Post a Comment