Social Icons

rss feed facebook twitter google plus linkedin youtube email

Thursday, November 29, 2012

Wimbi la mashambulio ya kigaidi nchini Iraq


Wimbi la mashambulio ya kigaidi nchini IraqJumanne tarehe 27 Novemba ilikuwa siku ya umwagaji damu mkubwa kwa Iraq na Wairaqi. Milipuko minane iliitikisa miji mbalimbali ya ya nchi hiyo na kwa akali watu 29 walipoteza maisha yao na zaidi ya mia moja na ishirini kujeruhiwa. Miji ya Kirkuk, Al Anbar na Baghdad ndiyo iliyolengwa na magaidi hapo jana. Polisi ya Iraq imelinyooshea kidole cha tuhuma kundi la mtandao wa al-Qaeda. Hata hivyo al-Qaeda ambalo ni kundi lililolelewa na Marekani, ni moja tu kati ya makumi ya makundi ya kigaidi ambayo yanaendesha harakati zao nchini Iraq. Inapaswa pia kuongeza katika majimui hiyo, harakati za kisiasa zinazoipinga serikali ya Baghdad na Noury al-Maliki mwenyewe, Waziri Mkuu wa nchi hiyo. Ushirikiano wa makundi na harakati hizi za kisiasa na magaidi, hadi sasa umeandaa uwanja wa kutokea milipuko na operesheni kadhaa za kigaidi nchini humo. Ni jambo linaloeleweka wazi kuwa, mrengo wa al-Iraqiya unaoongozwa na Iyad Allawi, una uhusiano wa karibu na makundi amilifu ya kigaidi nchini Iraq. Nchi kama Saudi Arabia, Qatar na Jordan ambazo hazifurahishwi na muundo wa kisiasa wa Iraq na hata Waziri Mkuu Noury al-Maliki, daima zimekuwa zikiuunga mkono mrengo wa al-Iraqiya na makundi amilifu ya kigaidi katika nchi hiyo na kuyapatia misaada ya kila upande. Nchi hizo, zimekuwa zikiutumia mrengo huo kama wenzo wa mashinikizo dhidi ya al-Maliki na ikilazimu walitumie kundi hilo kutoa pigo kwa serikali ya Baghdad na hivyo kuutilia alama ya swali utendaji wa al-Maliki. Hadi sasa makumi ya magaidi ambao ni raia wa Saudia, Imarati na Jordan wametiwa mbaroni. Huu ni ushahidi kwamba, Iraq inakabiliwa na njama kali pia kutoka kwa baadhi ya nchi za Kiarabu.    Nchi hizi za Kiarabu ambazo aghlabu zina uhusiano baridi na Iraq daima zimekuwa zikihesabiwa kuwa tishio kwa uthabiti wa kisiasa na kiusalama wa nchi hiyo. Pamoja na hayo, akthari ya weledi wa masuala ya kisiasa wanaamini kwamba, kuibuka wimbi jipya la machafuko huko Iraq bila shaka kutakuwa na uhusiano wa namna fulani na matukio ya Mashariki ya Kati yakiwemo ya Syria. Jumanne ya jana magari manane yaliyotegwa mabomu ndani yake yaliripuka katika miji mbalimbali ya nchi hiyo. Syria nayo ilikuwa na hali kama hiyo hiyo. Hii inaonesha kuwa, kuna njama za pamoja ambazo zinatekelezwa dhidi ya nchi hizo. Inaonekana kuwa, mamluki wa nchi za Kiarabu na makundi ya kigaidi ambayo yanapatiwa misaada ya kifedha na silaha na mhimili wa pamoja wa Kimagharibi-Kiarabu ulio dhidi ya Syria unataka kuishughulisha Iraq na Syria kwa migogoro ili uweze kunufaika na anga hiyo kwa maslahi yake. Iraq ni miongoni mwa nchi za eneo la Mashariki ya Kati ambazo hadi sasa zimekataa kuungana na mhimili ulio dhidi ya Syria.  Hapana shaka kuwa, jambo hilo limeikasirisha mno Marekani na baadhi ya nchi za Kiarabu ambazo ziko pamoja na Washington katika kadhia ya Syria. Wachambuzi wa masuala ya kisiasa wanaamini kuwa, moja ya sababu za kuzusha machafuko na sokomoko nchini Iraq ni kutaka kuilazimisha nchi hiyo ikubaliane na matakwa ya nchi za Magharibi kuhusiana na migogoro ya Mashariki ya Kati.

No comments:

Post a Comment