Social Icons

rss feed facebook twitter google plus linkedin youtube email

Tuesday, November 6, 2012

Naibu Mufti Mkuu azungumza na waandishi kuhusu kumwagia tindikali kwa Sheikh Soraga


Naibu Mufti Mkuu wa Zanzibar Sheikh Mahmoud Mussa Wadi amesema kitendo cha kumwagiwa Tindikali Katibu wa Mufti Mkuu Sheikh Fadhili Soraga si kitendo cha kiungwana na hakiendani kabisa na utamaduni na mila ya dini ya kiislamu .

Hayo ameyasema leo huko Ofisini kwake Mazizini nje kidogo ya Mji wa Zanzibar wakati alipokutana na waandishi wa habari kufuatia tukio la kujerihiwa vibaya katibu huyo kwa kumwagiwa tindikali na watu wasio julikana katika maeneo ya Kwerekwe kwenye kiwanja cha mpira alipokuwa akirudi mazoezi alfajiri ya leo.

Amesema kitendo hicho sio cha kiungwana na hakiendani na maadili ya uislamu kwani dini ya kiislamu siku zote ina amrisha kutenda mema na kukatazana Mabaya . “Uislamu ni Dini ya amani, upendo na kuaminiana na hawi mmoja wenu muumini wa kweli mpaka ampendelee mwenzake mema”alisema Naibu Mufti .

Aidha alifahamisha kuwa waliofanya kitendo hicho wafahamu kuwa wamefanya jambo baya na kama wanahisi kuwa Sheikh Soraya amefanya kosa wajibu wao ni kumwita na kumuelekeza kama dini ya kiislamu inavyosisitiza.

Amesema bila shaka hizo ni chuki binafsi na sio masuala ya uislamu na si vizuri kumuhusisha mtu na jambo lolote bila ya kufanya uchunguzi kwani unaweza kumfikiria mtu jambo ambalo halimhusu .

Alieleza kuwa kujeruhiwa kwa Sheikh Soraga ni mbinu za makusudi zilizoandaliwa na watu kwani awali aliwahi kufuatwa na maadui zake akitokea Mazizini kuelekea Malindi lakini walipofika Hailesalases dereva wake alibaini kuna gari inawafuata na aliamua kubadili njia na kupita Bustani ya Jamuhuri na maadui hawo wakatoweka.

Hata hivyo Naibu Mufti alisema dereva huyo hakuweza kuitambua gari ambayo ilikuwa ikiwafuata. Sheikh Soraya ameathirika sehemu ya usoni, kifuani na tumboni na hali yake ina endelea vizuri na amepelekwa Dar es Salamu katika Hospitali ya rufaa ya Muhimbili kwa matibabu .

No comments:

Post a Comment