Social Icons

rss feed facebook twitter google plus linkedin youtube email

Sunday, November 18, 2012

Mkutano wa Ziwa Nyasa waendelea nchini Tanzania



Mkutano wa Ziwa Nyasa waendelea nchini TanzaniaMkutano kati ya Tanzania na Malawi wa kujadili suluhu ya mgogoro wa mpaka kwenye Ziwa Nyasa umeingia siku yake ya pili jijini Dar es Saalam huku washiriki wakitoa mapendekezo mbalimbali kuhusu jinsi ya kuutafutia ufumbuzi mgogoro huo. Mkutano huo unaowahusisha wataalamu kutoka Wizara na Idara mbalimbali za Serikali za Tanzania na Malawi, unatarajia kuandaa mazingira ya kufanyika mkutano wa ngazi ya mawaziri baadaye hapo kesho. Akifungua Mkutano huo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa wa Tanzania, Bw. John Haule alisisitizia umuhimu wa wajumbe kutoka nchi zote mbili kujadili na kupendekeza njia zitakazosaidia kupata suluhisho la kudumu la mgogoro huo. Aidha, Bw. Haule aliweka bayana kuwa serikali ya Tanzania ina dhamira ya dhati kufanya kazi pamoja na serikali ya Malawi kutafuta suluhu ya mgogoro huo jambo ambalo pia lilisisitizwa na Bw. Julius Chisi, Kiongozi wa Ujumbe wa Malawi. Mazungumzo kati ya nchi mbili hizo yalivunjika mwezi Septemba baada ya Tanzania kutangaza ramani mpya ya nchi hiyo. Malawi ilijiondoa kwenye mazungumzo hayo kwa madai kwamba ramani hiyo mpya ya Tanzania inajumuisha eneo la Ziwa Nyasa linaloendelea kuzozaniwa na pande mbili hizo.

No comments:

Post a Comment