Social Icons

rss feed facebook twitter google plus linkedin youtube email

Sunday, November 11, 2012

Ukusanyaji silaha wafanyika magharibi mwa Ivory Coast


Ukusanyaji silaha wafanyika magharibi mwa Ivory Coast
Wapiganaji wa zamani huko magharibi mwa Ivory Coast wamekabidhi silaha zao katika oparesheni ya kukusanya silaha zisizokuwa na kibali nchini humo.  Oparesheni ya kukusanya silaha za aina hiyo ilianza katika nchi hiyo ya magharibi mwa Afrika mwishoni mwa mwezi Oktoba mwaka huu na inatazamiwa kumalizika tarehe 11 mwezi huu wa Novemba.
Viongozi wa serikali wamesisitiza kuwa wale wote wanaomiliki silaha kinyume cha sheria wanaweza kukabidhi silaha na zana za kijeshi walizonazo bila ya kuhofia kushtakiwa. Mtu ambaye atakabidhi silaha zake kwa hiyari kwa serikali atapewa franga 3000 ambazo ni sawa na dola sita. Kitendo cha kuwalipa fedha wale wote watakaokabidhi silaha zao ni hatua ambayo imechukuliwa na serikali ya Kodivaa ili kuwashawishi wamiliki silaha kinyume cha sheria wakabidhi silaha hizo.
Silaha nyingi na zana za kivita zilitumbukia mikononi mwa raia wa Kodivaa wakati wa vita vya ndani nchini humo kati ya mwaka 2010 hadi 2011. Kusalia silaha hizo mikononi mwa raia na makundi ya wanamgambo ni moja ya sababu za kuweko ukosefu wa amani na machafuko huko Ivory Coast. Mzozo wa kuwania madaraka kati ya mahasimu wawili wa kisiasa huko Ivory Coast ulioibuka mwezi Novemba miaka miwili iliyopita ulizusha mapigano kati ya wafuasi wa viongozi hao na kusababisha mgogoro mkubwa kote nchini humo. Hatua ya Laurent Gbagbo, Rais wa zamani wa nchi hiyo ya kupinga matokeo ya uchaguzi ilikuwa chanzo kikuu cha kuzuka mgogoro na machafuko ya umwagaji damu baada ya uchaguzi wa rais. Alassane Ouattara Waziri Mkuu wa zamani wa nchi hiyo ambaye alishinda katika duru ya pili ya uchaguzi wa rais mwezi Novemba mwaka 2010 alitambuliwa na Jumuya ya kieneo ya Ecowas na Umoja wa Afrika kuwa ndiye mshindi katika uchaguzi huo. Nchi mbalimbali na taasisi za kimataifa kama Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa pia zilimuunga mkono Ouattara baada ya kuthibitishwa kuwa mshindi na wakuu wa nchi za Magharibi mwa Afrika katika Jumuiya ya Ecowas.
Pamoja na hayo, Laurent Gbagbo ambaye alikuwa akiungwa mkono na baadhi ya vikosi vya jeshi alipinga matokeo hayo ya uchaguzi na kwa mara nyingine tena Ivory Coast ikatumbukia katika mgogoro.  Vilevile kuliripotiwa pia ukiukaji mkubwa wa haki za binadamu na kuuliwa raia wengi katika kipindi cha mwezi Novemba mwaka 2012 hadi Aprili 11 mwaka jana.

Wachambuzi wa masuala ya kisiasa wanaamini kuwa mauaji ya hivi karibuni na mashambulizi yaliyofanywa katika vituo vya jeshi la Ivory Coast yametekelezwa na wafuasi wa rais wa zamani wa nchi hiyo Laurent Gbagbo. Japokuwa baadhi ya ripoti za watetezi wa haki za binadamu zimewatuhumu pia wafuasi wa Alassane Ouattara kuwa walikiuka haki za binadamu wakati wa vita vya ndani nchini humo.
Kwa vyovyote vile zoezi la kukusanya silaha zinazomilikiwa kinyume cha sheria na wapiganaji wa zamani linahesabiwa kuwa hatua ya awali katika njia ndefu ya kurejesha utulivu na amani huko Ivory Coast.

No comments:

Post a Comment